Mazishi ya Fisi
Elizabeth Laird
Jacob Kono

Siku moja, mtoto wa fisi alifariki.

1

Punda mmoja alikimbia kuwajulisha jamaa zake.

Punda wengine waliuliza, "Mtoto wa fisi? Hiyo ni habari njema. Fisi wote ni maadui zetu."

2

Punda mmoja mzee alisema, "Ndugu zangu, lazima tuhudhurie mazishi tuonyeshe heshima."

Punda wengine wakauliza, "Eti nini? Tuhudhurie mazishi ya fisi? Hatutaki kwenda. Tunaogopa kuliwa na fisi."

3

"Sikiliza. Tusipoenda, fisi watakasirika sana. Watakuwa na sababu ya kutufanya kitoweo chao." Punda mzee alisema.

"Umesema ukweli. Lazima tuhudhurie mazishi ya fisi. Tukihudhuria, fisi watafurahi. Labda watakuwa marafiki zetu." Punda wengine walisema.

4

Fisi waliwaona punda nje ya nyumba yao. "Mbona punda wako hapa? Wamekuja kutucheka?" Fisi walijiuliza.

Punda walipowasikia fisi, waliogopa, wakaanza kuimba.

5

Wimbo ulienda hivi:

"Fisi wakubwa, mnawinda usiku kucha. Tunawasikia usiku wa manane. Meno yenu ni marefu. Macho yenu yanang'ara. Ingawa chakula chenu ni cheusi, kinyesi chenu ni rangi nyeupe. Sasa mmoja wenu amefariki!"

6

Mjombake fisi aliyekufa pia akawajibu kwa wimbo:

"Wimbo wenu ni mzuri. Maneno yenu ni matamu. Karibuni, wapendwa.
Lakini mmetuletea nini cha kula? Fisi wana njaa.
Wanahitaji nyama!"

7

Punda sasa waliogopa sana. "Hebu tutoroke," mmoja wao alisema. Mwingine alijibu, "Hatuwezi. Fisi watatukimbiza."

8

Punda mzee alishauri, "Tumekuja kuonyesha heshima zetu kwenu. Tunasikitika kwamba mtoto wenu amefariki. Tutaomba Mungu awafariji. Sasa lazima turudi nyumbani kwetu."

9

Fisi walisema, "Subiri! Hamuwezi kuondoka. Lazima mtupatie kitu cha kula. Tukatieni midomo yenu."

10

Punda waliangaliana. "Pengine tukiwakatia midomo yetu, watatuachilia twende." Waliwaza.

11

Fisi walikata midomo ya punda wakala.

12

Kwa mara nyingine, punda waliomba kuruhusiwa kuondoka.

13

"Ndugu zangu, mtawaacha hawa punda waende?
Waangalieni! Tunaweza kuyaona meno yao! Wanatucheka!"

14

Fisi waliwarukia punda wakawaua halafu wakaanza kuwala.

15

Kabla punda mzee kufa, aliwatazama fisi akasema, "Fisi waovu, tulikuja kwa wimbo kuwafariji lakini tulikosea! Mkiwa na njaa, msitafute sababu ya
kuwala marafiki zenu!"

16
You are free to download, copy, translate or adapt this story and use the illustrations as long as you attribute in the following way:
Mazishi ya Fisi
Author - Elizabeth Laird, Yirga Ejigu
Translation - Brigid Simiyu
Illustration - Jacob Kono
Language - Kiswahili
Level - Longer paragraphs