

Parna alikuwa mvulana mwembamba mrefu. Alikuwa katika darasa la tatu.
Alipenda kuvaa koti refu la rangi nyeusi. Alipewa koti hilo na Mjombake, Teteyo.
Wakati wa likizo, Parna aliwachunga ng'ombe wa wazazi wake.
Siku moja, Parna alikuwa akiwachunga ng'ombe. Ghafla, mvua ilianza kunyesha.
Wakati huo huo, Cheusi, ng'ombe aliyekuwa kipenzi cha babake, alizaa.
Ndama aliyezaliwa alipendeza. Alikuwa mzuri kuliko ndama wote ambao Parna aliwahi kuwaona.
Parna alifurahi kuwahudumia Cheusi na ndama wake. Aliwasahau ng'ombe wale wengine.
Aliwaza, "Babangu aliahidi kunipa ndama ikiwa atakuwa wa kike."
Alipokuwa akiwaza hivyo, alisikia mkono ukimvuta juu kwa nguvu.
Parna alimwona Mjomba Teteyo. Alikumbuka na kuuliza, "Mjomba, ng'ombe wako wapi?"
Mjomba Teteyo alimjibu, "Mamako aliwapata ng'ombe wote zizini ila wewe na Cheusi. Aliingiwa na wasiwasi akanituma nije nikuchukue."
Mjomba Teteyo akasema, "Nitambeba ndama huyu. Kisha wewe na Cheusi mnifuate nyuma."
Parna alielezea kwa msisimko jinsi Cheusi alivyozaa ndama aliye mzuri zaidi ya wote.
Watu wote walifurahi walipoona kwamba Parna, Cheusi na ndama walikuwa salama.
Parna akamwuliza babake, "Je, utanipa ndama huyu kama ulivyoahidi?"
"Ndiyo, mwanangu, ndama huyu ni wako. Ahadi ni deni."

