Tamara aanza kwenda shule
Soila Murianka
Jacob Kono

Tamara alikuwa msichana wa miaka mitano.

Aliishi na familia yake karibu na msitu wenye wanyama wakali.

1

Tamara aliwatii wazazi wake.

Aliwasaidia kuwachunga kondoo na mbuzi wao.

2

Tamara alipenda kuwasikiliza ndege wakiimba.

Walipoimba, aliwaiga huku akitunga nyimbo zake.

3

Kwa sababu ya umri wake mdogo, Tamara hakuwa ameanza kwenda shule.

Nashipae na Tasieku walikwenda kwa sababu walikuwa wakubwa.

4

Nashipae, Tasieku na watoto wengine kutoka kijijini walienda pamoja asubuhi na kurudi jioni.

Walikuwa wakibeba chakula katika mikebe midogo.

5

Siku moja, Tamara alimwuliza mamake, "Je, nitaanza kwenda shule lini?"

Mama alimjibu, "Utaenda hivi karibuni mwanangu mpendwa."

6

Siku moja, chifu na wenzake walifika nyumbani kwa gari.

Lilikuwa jukumu la chifu kuhakikisha kwamba watoto walienda shule walipofikisha umri uliokubaliwa.

7

Watu waliamini kwamba mtoto akiweza kuunyoosha mkono wake kupita kichwani na kulishika sikio lake, mtoto huyo yuko tayari kuanza kwenda shule.

8

Chifu alimwuliza Tamara, "Una umri wa miaka mingapi?"

Tamara alimjibu, "Mitano."

"Hebu tuone ikiwa unaweza kwenda shule," chifu alisema.

9

Mmoja wa wanawake wale aliuchukua mkono wa kulia wa Tamara akauweka kichwani kwake.

Tamara aliweza kulishika sikio lake la kushoto.

10

Waliamua kwamba wakati ulikuwa umefika wa Tamara kuanza kuhudhuria shule.

Angeanza kwenda shule iliyokuwa karibu na nyumbani kwao.

11

Tamara alifurahi sana akawaza, "Nitajua kusoma na kuandika kama Nashipae na Tasieku wafanyavyo."

12
You are free to download, copy, translate or adapt this story and use the illustrations as long as you attribute in the following way:
Tamara aanza kwenda shule
Author - Soila Murianka
Translation - Ursula Nafula
Illustration - Jacob Kono
Language - Kiswahili
Level - First sentences