Anansi awapa watu hadithi
Ghanaian folktale
Wiehan de Jager

Hapo zamani za kale, Mungu wa hadithi, alizifungia hadithi zote kwenye sanduku la mbao, huko juu.

Watu duniani walihuzunika sana kwa kuwa hawakuhadithiana.

Wakamwuliza Buibui Anansi, mwerevu, awasaidie.

1

Buibui Anansi alisokota utando mrefu unaonata, akautumia kupanda hadi mbinguni.

"Tafadhali nipe hadithi?" Buibui Anansi alimwambia Mungu wa hadithi.

Lakini Mungu wa hadithi alimcheka Anansi akisema, "Hadithi hizi ni ghali mno. Wewe buibui mdogo hutaweza kuzilipia."

2

"Hadithi hugharimu pesa ngapi?" Buibui Anansi aliuliza."

"Itabidi uniletee wanyama watatu wakali tena wa kipekee. Chui mwenye meno makali kama mkuki, nyigu anayewauma watu, na nyoka anayewameza watu," Mungu wa hadithi alisema.

Alicheka tena. Alidhani kwamba hadithi zake zilikuwa salama.

3

Buibui Anansi alishuka chini polepole. Aliwaza na kuwazua kisha akapata mpango.

Alichimba shimo refu, akalifunika kwa matawi na udongo ili lisionekane, halafu, akaenda nyumbani.

Asubuhi iliyofuata, chui alikuwa ameanguka kwenye lile shimo. Alikuwa akikwaruza kuta za shimo kwa hasira.

4

"Hebu nikusaidie, rafiki yangu. Lala juu ya vijiti hivi halafu nitakuvuta utoke nje," Buibui Anansi alisema.

Buibui Anansi akautungia utando wake unaonata kwenye mwili wa chui na vijiti. Akamvuta hadi juu kwa Mungu wa hadithi.

Lakini, Mungu wa hadithi alimcheka akauliza, "Wako wapi nyigu na nyoka?"

5

Buibui Anansi alirudi tena ardhini kumtafuta mnyama wa pili. Alifikiri hatimaye akapata wazo. Alichukua kibuyu kilichojaa maji na kwenda kwenye mti walimoishi nyigu.

Akamwagilia nyumba ya nyigu maji mpaka ikalowa kabisa. Kisha akatafuta jani la mgomba akajikinga nalo kichwani. Akajimwagilia maji yaliyobaki kila sehemu ya mwili.

6

Akawaita nyigu, "Aisee nyigu! Njooni mwone! Mvua inanyesha! Ingieni haraka ndani ya kibuyu changu ili mjikinge na mvua."

Nyigu hawapendi kulowa maji. Walikimbilia ndani ya kibuyu cha Buibui Anansi.

7

Kwa kasi, Buibui Anansi aliutungia utando wake kwenye mlango ili nyigu wasitoke kamwe.

Akawabeba wote hadi juu kwa Mungu wa hadithi. Lakini, Mungu wa hadithi alisema, "Wapi nyoka?"

Wakati huu hakucheka.

8

Kwa hivyo, Buibui Anansi alirudi ardhini tena. Alifikiri lakini hakuna wazo zuri lililomjia akilini.

Basi akamwuliza mkewe aliyekuwa na wazo bora sana. Walishirikiana kutafuta kijiti kimoja kirefu na kamba dhabiti.

Walipofika karibu na mto alimoishi nyoka, walianza kubishana.

9

Mmoja alidai kuwa kijiti kile kilikuwa kirefu huku mwingine akisema sivyo.

Nyoka alitoka majini akawauliza sababu ya mabishano yao. "Mke wangu anasema kwamba kijiti hiki ni kirefu kukuliko wewe. Lakini si kweli," Buibui Anansi alisema.

"Mimi ni mrefu kuliko kijiti hicho! Hebu kiweka karibu nami nijipime," nyoka alijibu.

10

Buibui Anansi alifanya hivyo. Alimfunga yule nyoka kwenye kijiti kile kwa kutumia kamba ili kumnyoosha sawasawa.

Alimbeba hadi juu mbinguni.

11

Mungu wa hadithi akaridhika na malipo ya Buibui Anansi.

Akafungua sanduku lake la mbao, akampa Buibui Anansi hadithi. Buibui Anansi alizigawa kwa mkewe, watu pamoja na wanyama.

Hadithi ni za kuhadithia wala si za kuficha sandukuni.

12
You are free to download, copy, translate or adapt this story and use the illustrations as long as you attribute in the following way:
Anansi awapa watu hadithi
Author - Ghanaian folktale
Translation - Mutugi Kamundi
Illustration - Wiehan de Jager
Language - Kiswahili
Level - Read aloud