Mwanamume aliyekuwa na tatizo kubwa
Ursula Nafula
Abraham Muzee

Munia aliishi na babu, bibi, shangazi na mjomba. Alifuga kuku, mbuzi, kondoo na nguruwe. Wote walikaa kwenye chumba kimoja.

Kuku alikuwa na kitundu chake. Mbuzi, kondoo na nguruwe walifungwa pembeni.

Bibi na babu walikuwa bado na afya nzuri. Shangazi na mjomba walisaidia kufanya kazi za pale nyumbani.

1

Hata hivyo, mambo yalibadilika miaka michache baadaye. Bibi na babu walizeeka na hawakuweza kusikia wala kuona vizuri.

Shangaziye aliugua na hakuweza kusaidia katika usafi wa nyumba.

Mjombake alilala wakati wote na hakusaidia katika shughuli za kuwalisha wanyama.

2

Wanyama walipiga kelele nyingi kwa sababu walikuwa na njaa. Nyumba pia ilikuwa chafu kwa sababu shangazi hakuweza kuisafisha.

Munia alikuwa mchovu wakati wote. Alitoka kila siku kuwatafutia wote chakula.

3

Munia hakuweza kukabilina na hali hiyo tena. Aliwandea babu na bibi kuwauliza suluhisho. Lakini, alihuzunika sana kwa sababu aliondoka bila suluhisho kwani hawakuweza kumsikia.

Shangaziye mgonjwa alisema, "Ninachohitaji ni kuweza kulala usiku na kuamka asubuhi."

4

Mjombake mzembe alisema, "Wauze wanyama hawa kisha ukawanunulie chakula. Watalala wakome kukusumbua."

Munia alisema kwa hasira, "Mjomba, unajua kwamba siwezi kuwauza wanyama hawa. Wao pekee ndio mali yangu."

5

Usiku mmoja, Munia hakupata usingizi. Alimkumbuka mtu mmoja aliyekuwa na busara. Mtu huyo aliaminika kuyajibu maswali yote na kusuluhisha matatizo yote.

Munia aliwachukua wanyama wake akaenda nao kumtembelea mtu yule. Aliwafunga mbuzi, kondoo na nguruwe kwa Kamba kisha akambeba kuku.

6

Munia alifika nyumbani kwa mtu huyo akiwa amechoka na mwenye njaa sana. Baada ya kueleza shida yake, mtu huyo alisema, "Nitakusaidia, lakini ni sharti ufanye nikuambiavyo."

Munia alijibu, "Nitafanya chochote kusuluhisha tatizo langu."

7

Mtu yule alimwambia, "Waache wanyama hapa kisha urudi nyumbani."

Munia alisema, "Nimeishi na wanyama hawa kwa muda mrefu. Wao ndio mali pekee niliyo nayo."

8

Mtu akajibu, "Nilikuambia nitakusaidia lakini ni lazima ufanye nikuambiavyo."

Kwa vile Munia alihitaji suluhisho kwa tatizo lake, aliwaacha wanyama akarudi nyumbani.

9

Nyumba yake ilikuwa na kimya kingi na ilikuwa tupu. Babu na bibi walilalamika kwamba hawakupata maziwa kutoka kwa mbuzi.

Mjombake alisema, "Tumekuwa maskini sana, kila mtu anatucheka."

10

Munia hakuweza tena kuvumilia malalamishi yao. Pia, aliwakosa wanyama wake.

Alirudi kwa mtu yule mwenye busara ili kumwuliza mawaidha. "Maisha yangu yamekuwa fotauti bila wanyama wangu. Jamaa zangu wanalalamika kila wakati."

11

Mtu yule alimwambia, "Nitakusaidia, lakini, ni lazima ufanye nikuambiavyo. Nenda nyumbani kisha uwatoe nje bibi na babu kutoka kwenye nyumba."

Munia alimjibu, "Nitawezaje kufanya hivyo? Wao ni wavyele wangu na wananitegemea."

12

Mwishowe, Munia alienda nyumbani akafanya alivyoambiwa. Hakuweza kupata amani akilini mwake.

Babu na bibi hawakuwa na mahali pa kuenda. Walirandaranda wakiangukia miti na kuhisi baridi usiku.

13

Shangaziye mgonjwa alilia akisema, "Tafadhali usinitupe nje."

Mjombake mzembe alisema, "Sitaondoka kitandani usije ukanitupa nje pia."

14

Munia hakuweza kustahimili mambo haya hata kidogo. Alirudi kwa mtu mwenye busara akiwa amechanganyikiwa na mwenye hasira.

Alimlilia akisema, "Mambo haya ni magumu sana kwa mtu mmoja. Nipe suluhisho bora zaidi."

15

Mtu mwenye busara alisema, "Hapa, wachukue wanyama wako na uwarudishe bibi na babu kwenye nyumba pia."

Munia alifanya alivyoambiwa. Shangaziye alisema, "Nitasafisha nyumba kwa bidii."

Mjombake aliacha kuwa mzembe akamsaidia Munia na kazi za nyumbani. Wakaishi kwa furaha tena.

16
You are free to download, copy, translate or adapt this story and use the illustrations as long as you attribute in the following way:
Mwanamume aliyekuwa na tatizo kubwa
Author - Ursula Nafula
Translation - Susan Kavaya
Illustration - Abraham Muzee
Language - Kiswahili
Level - Read aloud