

Zamani, Moto, Maji, Ukweli na Uongo walikuwa marafiki.
Uongo hakufurahia urafiki huo.
Alitafuta njia ya kuuvunja.
Siku moja Uongo alisema, "Tuitafute nchi huru ili kila mmoja wetu amiliki ufalme wake."
Walikubaliana wakaanza kutafuta nchi huru.
Uongo alimwambia Maji, "Moto ni adui yetu mkubwa. Yeye huunguza kila kitu. Tutafute ufalme ambako Moto hatakuweko."
Maji akauliza, "Tutafanyaje?"
Uongo akamjibu, "Ni wazi kwamba tutamuua. Ni wewe tu uliye na uwezo wa kufanya hivyo. Atakapokuwa ameketi chini, jimwagilie kwake umharibu!"
Maji alisema, "Nikifanya hivyo nitaenea kila mahali. Sitaweza kujikusanya tena."
Uongo alisema, "Hilo si tatizo. Nitayaweka mawe chini yakuzuie kuenea, kisha nitakukusanya tena."
Uongo alifanya hivyo.
Moto alipokuwa ameketi chini, Maji alijimwaga kwake bila Moto kujua. Kupitia njia hiyo, Uongo aliweza kumwangamiza Moto.
Yeye na Maji waliendelea na safari yao.
Baada ya muda, Uongo alimwambia Maji, "Hebu keti juu ya ukingo huu ili uyafurahie mandhari haya."
Maji alipokuwa ameketi chini, Uongo aliyaondosha mawe yaliyomzingira.
Maji alimwagika akatapakaa kila mahali. Huo ndio ulikuwa mwisho wake.
Sasa Uongo alilazimika kumwangamiza Ukweli.
Walipofika kwenye mlima mkubwa, Uongo alimweleza Ukweli asubiri chini ya mlima.
Kisha Uongo akalisukuma jiwe kubwa kutoka juu kumwangamiza Ukweli.
Jiwe lilipoporomoka chini, almasi, dhahabu na vito tofauti vya thamani vilipatikana.
Ukweli aliweza kujivuta na kutoka chini ya jiwe lililokuwa limevunjika.
Uongo alishuka chini kutazama mwili wa Ukweli. Badala yake, aliona vito vya thamani.
Akauliza, "Vito hivi vimetoka wapi?"
Ukweli alijibu, "Jiwe liliponiangukia, vito hivi vilimwagika." Uongo pia alitaka vito hivyo vya thamani.
Alisema, "Nitaenda chini ya mlima nawe uende juu uliangushe jiwe jingine kubwa."
Basi, Ukweli akapanda juu ya mlima akalisukuma chini lili jiwe kubwa.
Jiwe hilo lilimwangukia Uongo kichwani.
Akafa papo hapo.
Hata hivyo, Uongo hubishana na Ukweli kila siku.

