

Eba na mkewe Lelisa walifanya kazi zao kwa bidii sana.
Walikuwa na watoto wawili wa kiume.
Walitimiza mahitaji yao kutokana na juhudi zao.
Eba alitaka wanawe wastarehe. Hawakufanya kazi zozote.
Baada ya muda, Lelisa alifariki.
Hata baada ya kifo cha mkewe, Eba hakutaka wanawe wamsaidie.
Alizifanya kazi zote za shambani na za nyumbani.
Eba alizeeka na kudhoofika. Alihofia maisha ya wanawe.
Alijiuliza, "Wanangu wataishi namna gani nitakapofariki?"
Alijua kuwa hawangeweza kujitegemea.
Eba aliwaita wanawe akawaambia, "Urithi mtakaopata kutoka kwangu ni dhahabu nyingi iliyofichwa shambani. Ni juu yenu kuyalima mashamba ili muipate dhahabu hiyo."
Eba pia aliwaambia majirani, "Nadhani niko karibu kufariki. Wanangu hawajui kujitegemea. Nawasihi mwasaidie hadi watakapoweza kujikimu wenyewe."
Baada ya Eba kufariki, majirani waliwapa wanawe chakula kwa muda.
Ndugu hao hawakutaka kuporwa dhahabu iliyofichwa na baba yao.
Waliamua kuyalima mashamba wenyewe ili waipate dhahabu hiyo.
Waliyalima mashamba moja baada ya jingine.
Ila, hawakupata dhahabu yoyote.
Mmoja alimwuliza mwingine, "Je, unadhani baba alitudanganya?"
Yule akajibu, "La, ninadhani baba alikuwa na maana kuwa ukulima ni dhahabu."
Kwa hivyo, kama wakulima wengine, wana hao waliyalima mashamba yao.
Walipanda mimea wakawa matajiri sana.

