

Siku moja Sungura alienda kutafuta chakula. Alikutana na Tembo akibeba asali mgongoni.
Sungura alimwambia Tembo, "Tafadhali nibebe. Mimi ni mnyonge."
Tembo alikubali Sungura akadakia mgongo wake.
Sungura alianza kula asali ya Tembo!
Asali ilianza kudondoka.
Tembo alipouliza, Sungura alisema kuwa yalikuwa maji yaliyotoka kwenye kidonda chake.
Waliufikia mto na kumkuta Kiboko akinywa maji.
Sungura alitaka kujua kati ya Tembo na Kiboko, ni nani aliyekuwa na nguvu kumshinda mwingine.
Walianza kubishana.
Tembo alisema yeye ndiye mwenye nguvu zaidi naye Kiboko akasema ni yeye.
Sungura alisema kuwa alijua jinsi ya kutambua aliyekuwa na nguvu zaidi.
Aliwaambia wamsubiri.
Sungura alirudi na kamba ndefu.
Alimfunga Tembo kiunoni na kumwelekeza mbali na mto.
Kisha Sungura akamfunga Kiboko kiunoni na kumuacha pale karibu na mto.
Sungura alijificha mtini akawaambia, "Tayari! Moja, mbili, tatu! Vuta sasa!"
Kiboko na Tembo walivutana.
Tembo akamvuta Kiboko naye Kiboko akamvuta Tembo.
Kiboko na Tembo wakavutana lakini, hakuna aliyeweza kushinda.
Sungura aliendelea kula asali ya Tembo kule mtini.
Alipomaliza kuila asali, aliikata kamba karibu sana na Kiboko.
Tembo aliuangukia mti kwa kishindo.
Sungura alimshangilia Kiboko akisema kwamba yeye ndiye mwenye nguvu zaidi.

