

Katika msitu wa Miwa, aliishi Kima aliyehuzunika.
Kila alipomzaa mtoto, aliaga dunia.
Uchungu wa kuwapoteza watoto ulimfanya Kima kuruka juu na chini.
Angeruka kutoka tawi moja hadi nyingine huku akilia, "Kwi! Kwi! Kwi!"
Kima alihuzunika zaidi alipowaona kima wengine wakiwa na watoto wao.
Kima mwenye huzuni alikuwa na tabia ya kuketi juu ya tawi na kutazama juu!
Siku zilivyopita, ndivyo Kima alilia zaidi na zaidi.
Baadaye, alimzaa mtoto mwingine.
Aliamua kumpeleka njiani ili watu wote waliopita wamwone na kumtakia heri.
Siku moja, Kima alishuka kutoka mtini na kumweka mtoto wake njiani.
Wakati huo, mwindaji mmoja alikuwa akirudi nyumbani. Alimwona mtoto wa Kima aliyelala kando ya njia.
Mwindaji huyo alimbeba mtoto wa Kima na kumpeleka nyumbani kwake.
Alipofika, kila mmoja wa wanawe watatu alitaka kumbeba mtoto wa Kima.
Walicheza na kuimba:
Mtupe juu!
Mtupe chini!
Nitupie mimi!
Mtupie yeye! Walimtupa mtoto wa Kima kutoka kwa mmoja hadi kwa mwingine.
Walipokuwa wakicheza na mtoto wa Kima, mama Kima alijificha mtini na kuwatazama.
Alihofia kwamba mwanawe angekufa kama vile wale wengine walivyokufa.
Mke wa mwindaji aliwaona wanawe wakicheza na yule mtoto wa Kima.
"Tahadharini wanangu! Hebu mleteni hapa. Mtamwangusha!" Akasema.
Alimshika mtoto wa Kima na kumbariki.
Kisha mke wa mwindaji alimweka mtoto wa Kima chini. Mama Kima akamchukua na kumbeba mtoto wake kifuani.
Halafu akatoweka mtini. Hakumpoteza tena mtoto mwingine!

