Anansi na Tai
Ghanaian folktale
Wiehan de Jager

Buibui Anansi, na Sungura, walikuwa marafiki. Waliishi kwa amani kijijini milimani. Sungura alimiliki shamba kubwa lililojaa mboga na matunda.

Ingawa Sungura alimgawia rafikiye Anansi kwa ukarimu, Anansi hakufurahia na alimwonea wivu.

1

Buibui Anansi aliwaza jinsi angelinyakua shamba la Sungura na kulifanya kuwa lake. Alifaulu na kumwacha Sungura katika hali ya umaskini na bila makao.

Buibui Anansi sasa alijivunia kuwa mmiliki wa shamba lote la Sungura pamoja na mboga na matunda.

2

Siku moja, Buibui Anansi alienda sokoni kuuza matunda na mboga. Alizipata hela nyingi akakijaza kikapu!

Alizitumia baadhi ya hela hizo kuinunulia familia yake nafaka. Aliweka nafaka hiyo juu ya hela zilizokuwa kikapuni.

3

Buibui Anansi alikibeba kikapu chake kichwani akaelekea nyumbani huku akiimba.

Wakati wote huo, alikuwa akiwaza juu ya vitu vyote ambavyo angetumia hela hizo zote kununa.

4

Alipokuwa njiani, kulikuwa na manyunyu ya mvua. Punde tu manyunyu yaligeuka na kuwa mvua kubwa iliyomwagika.

Buibui Anansi alikiacha kikapu chake pembeni mwa barabara naye akaenda chini ya mti kujikinga. Lakini alikichunga kikapu hicho cha thamani kutoka pale alikokuwa.

5

Mvua ilinyesha kwa wingi zaidi hadi Anansi akalowa na kuhisi baridi.

Aliamua kukimbilia shimoni. "Nitaketi hapa shimoni hadi mvua itakapoisha," alijiambia. "Bora hela zangu zimekingwa na nafaka niliyoweka juu yake."

6

Muda mfupi baadaye, Tai aliruka pahali pale na kukiona kikapu kando ya barabara. Aliona pia kwamba kulikuwa na fedha na nafaka.

Tai alikifunika kikapu hicho kwa mabawa yake na kusubiri mvua iishe.

7

Buibui Anansi alimwona Tai akiwa amekalia kikapu chake. "Ah asante rafiki yangu kwa kukilinda kikapu changu," alimwambia Tai.

"Samahani, Anansi, nilikusikia vyema?" Tai aliuliza. "Eti kikapu chako? Kikapu hiki ni changu! Nilikipata hapo pembeni mwa barabara!"

Buibui Anansi hakuweza kuamini masikio yake! "Ni changu, nakwambia!"

8

Buibui Anansi alienda kushtaki kwa Chifu. Tai aliwaambia Chifu na wazee, "Inawezekanaje kukiacha kikapu kilichojaa fedha na nafaka barabarani bila ulinzi wowote?"

"Nilikuwa nikikichunga kikapu changu. Fedha ni zangu na nafaka ni yangu!" Buibui Anansi alisema.

"Nilikuwa nimekikinga kikapu hiki kwa mabawa yangu ulipotokezea na kudai kwamba kilikuwa chako!" Tai alijibu.

9

Baada ya Chifu na wazee wake kusikiliza kwa makini pande zote mbili, waliwataka Buibui Anansi na Tai watoke hapo na kwenda mbali kidogo.

Walijadili kisa hicho kwa muda mrefu. Hatimaye, walifikia uamuzi.

10

Waliwaita tena Buibui Anansi na Tai. "Tunamwamini Tai," walisema. "Yeye si mwizi. Wewe Anansi, ulikuwa ukijitakia kitu kisichokuwa chako."

Buibui Anansi hakuweza kuamini masikio yake. Aliangua kilio.

11

Ujumbe ulisambaa kwamba uamuzi ulimwendea vibaya Buibui Anansi. Buibui Anansi alipoondoka, alimsikia Sungura akicheka kwa nguvu.

Sungura alirudi shambani kwake akaendelea kupanda matunda na mboga.

Buibui Anansi aliwapoteza marafiki wote. Alirejelea hali yake ya umaskini.

12
You are free to download, copy, translate or adapt this story and use the illustrations as long as you attribute in the following way:
Anansi na Tai
Author - Ghanaian folktale
Translation - Brigid Simiyu
Illustration - Wiehan de Jager
Language - Kiswahili
Level - Read aloud