

Kwenye msitu wa Miwa paliishi tumbili aliyekuwa na huzuni sana.
Kila alipozaa, mtoto wake alifariki.
Uchungu wa kufiliwa na watoto wake ulimfanya tumbili kuruka juu na chini.
Tumbili huyu alikuwa akirukia tawi hili hadi kwenye lingine. Alipiga mayowe, "Kwi! Kwi! Kwi! Kwi!"
Tumbili alikuwa na huzuni wakati wote.
Huzuni wake ulimzidi haswa alipowaona akina mama tumbili wengine na watoto wao.
Tumbili mwenye huzuni alijiwayawaya huku na huku. Alijiwayawaya kwenye tawi hili na lile!
Siku zilipita na tumbili alizidi kulia zaidi.
Halafu, alizaa tena.
Aliamua kumpeleka mtoto wake njiani ili wapita njia wamwone na kumtakia heri.
Tumbili alishuka na kumweka mtotowe njiani.
Wakati huo, mwindaji alikuwa akirejea nyumbani. Alimwona mtoto wa tumbili akilala kando ya njia.
Mwindaji alimbeba mwana tumbili hadi nyumbani kwake.
Alipofika nyumbani, wavulana wake watatu walifurahi kumwona mwana tumbili.
Watatu hao waliimba:
Mrushe juu!
Mrushe chini!
Mrushe kwangu!
Mrushe kwake!
Mwana tumbili alirushwa kutoka kwa mmoja hadi mwingine.
Wavulana wale walipoendelea kucheza na mwana tumbili, mama tumbili alijificha mtini na kuangalia.
Aliogopa kuwa mtoto huyu naye angefariki kama wengine.
Mara mke wa mwindaji aliwaona watoto wakicheza na tumbili mtoto.
Aliwaonya, "Kuwa waangalifu! Hebu mlete hapa. Mtamwangusha!"
Alimchukuwa mwana tumbili mikononi mwake na kumbariki.
Alipomweka mwana tumbili chini, mama tumbili alikimbia kwa furaha.
Alimbeba mwanawe kifuani na kwenda mtini.

