Kisirusiru, mjinga
Cissy Kiwanuka Luyiga
Catherine Groenewald

Hapo zamani za kale, kulikuwa na mkulima na mkewe.

Walikuwa na mtoto mmoja pekee mvulana aliyeitwa Kisirusiru.

1

Kisirusiru alipompeleka mbuzi malishoni, mbuzi alirarua shati lake. Mamake alimtuma sokoni kununua sindano aweze kushona shati lake.

Kisirusiru aliiweka sindano kwenye mfuko wa shati lake. Njiani, alijiunga na wavulana waliokuwa wakicheza mpira. Sindano ilipotea.

2

Kisirusiru alipofika nyumbani, alisema, "Samahani mama, nimepoteza sindano njiani."

"Mwanangu, wakati mwingine, idunge sindano kwenye karatasi kisha uiweke mfukoni," mamake alieleza.

"Ndiyo mama, nimeelewa," Kisirusiru alijibu.

3

Kisirusiru alichukua chungu kwenda mtoni. Alikifungia chungu ndani ya kipande cha karatasi. Alipokuwa njiani, karatasi iliraruka, chungu kikaanguka na kuvunjika vigae vigae. Maji yote yalimwagika.

Alipofika nyumbani, Kisirusiru alimweleza mamake, "Samahani mama, chungu kimevunjika."

"Mwanangu, wakati mwingine, kibebe chungu kichwani," mama alishauri.

"Ndiyo mama, nimeelewa," Kisirusiru alijibu.

4

Siku iliyofuata, babake alimtuma Kisirusiru ampeleke mbuzi malishoni. Kisirusiru alimbeba mbuzi kichwani. Mbuzi alimpiga mateke na kumkwaruza kichwa hadi damu ikamtiririka usoni. 

Babake alikereka akamwuliza, "Utaacha ujinga wako lini? Mbuzi hufungwa na kuvutwa kwa kamba! Usipokuwa mwerevu, utahama hapa nyumbani."

5

Siku iliyofuata, babake alimtuma akanunue nyama sokoni. Kisirusiru alikumbuka alivyoambiwa na babake.

Aliifunga nyama kwa kamba akaivuta kuelekea nyumbani. Alikimbia ili babake asisubiri kwa muda mrefu.

Hebu fikiria, nyama hiyo ilikuwaje alipowasili nyumbani?

6

Babake alikasirika mno akamwambia afunganye virago vyake ahame nyumbani.

Mamake aliposikia hivyo, aliamua kuondoka pamoja na mtoto wake.

Waliung'oa mlango wa jikoni wakaubeba ili wawe na kitu cha kuanzia ujenzi wa nyumba yao mpya.

7

Walitembea kwa muda mrefu. Lakini, hawakupata mahali pa kujenga nyumba yao mpya.

Giza lilipoingia, waliamua kukwea mti na kulala pale.

8

Kisirusiru na mamake waliamua kukaa juu ya mti. Walipokuwa wakiuvuta mlango juu, walisikia makelele chini.

Waliwaona wavulana watatu waliobeba magunia makubwa. Waliuachilia mlango ukaanguka kwa kishindo.

Kishindo kiliwaogofya wavulana wale wakaacha kila kitu na kutoroka.

9

Kisirusiru na mamake walishuka chini na kuyafungua yale magunia. Humo walipata pesa, nguo, mablanketi, na kila kitu walichohitaji kuanzisha nyumba yao.

Punde, walipata pahali pa kujenga nyumba. Waliishi kwa furaha tangu siku hiyo.

10
You are free to download, copy, translate or adapt this story and use the illustrations as long as you attribute in the following way:
Kisirusiru, mjinga
Author - Cissy Kiwanuka Luyiga
Adaptation - Brigid Simiyu
Illustration - Catherine Groenewald
Language - Kiswahili
Level - Read aloud