Demane na Demazane
South African Folktale
Jemma Kahn

Hapo zamani kuliondokea mvulana mmoja aliyeitwa Demane. Alikuwa na pacha mwenzake aliyeitwa Demazane.

Wazazi wao walipofariki, Demane na Demazane walienda kuishi na mjomba wao. Mjomba aliwachapa na kuwalisha uji mwepesi.

1

Walitorokea pangoni wakaishi kwa hofu nyingi. Majitu yaliishi karibu na pango hilo.

Waliunda mlango wenye mashimo mawili ya kupitisha hewa na mwangaza. Demane akamwambia dadake, "Baki humu pangoni nikatafute chakula. Kamwe usipike nyama. Majitu hupenda sana harufu ya nyama."

2

Kila jioni Demane alirudi na nyama na kuimba:

Demazane, Demazane
nimefika kwenye pango
nimewinda korongo
ufungue kwa mpango
asiingie muongo

Demazane alichoka kukaa pangoni peke yake. Siku moja alitembea na kupanda miti. Alifurahia akawaza, "Labda hakuna majitu."

3

Keshoye, alipata ukakamavu. Aliuwasha moto pangoni ili kuondoa baridi. Kwa kuogopa majitu, aliufunga mlango kabisa.

"Nina hakika hakuna hatari nikichoma nyama kwa moto huu. Chakula cha kuchomwa ni kitamu." Demazane aliwaza.

4

Demane aliimba:

Demazane, Demazane
nimefika kwenye pango
nimewinda korongo
ufungue kwa mpango
asiingie muongo.

Demazane alimwambia, "Nilichoma nyama hii kwenye jua nje ya pango." Kwa vile Demane alikuwa amechoka, hakuuliza maswali zaidi.

5

Siku iliyofuata, Demazane alichoma nyama tena. Alpomaliza, alisikia wimbo:

Demazane, Demazane
nimefika kwenye pango
nimewinda korongo
ufungue kwa mpango
asiingie muongo.

Demazane akasema, "Wewe si kakangu. Hiyo sio sauti yake."

6

Baada ya muda mfupi, aliskikia sauti tena ikiimba:

Demazane, Demazane
nimefika kwenye pango
nimewinda korongo
ufungue kwa mpango
asiingie muongo.

Sauti hiyo ilifanana sana na ya kakake. Demazane aliufungua mlango.

7

Jitu kubwa lenye nywele mwili mzima lilijaa mlangoni. Likamchukua Demazane haraka.

Kabla kuondoka, Demazane aliweza kuliokota jivu la jikoni na kulibeba. Walipokuwa wakienda, alimimina jivu lile njiani walikopitia.

8

Demane aliporudi, alipata mlango ukiwa wazi na Demazane hakuwa ndani.

Lakini, aliona jivu lililomwagwa kulekea msituni.

Alifuata jivu hilo mpaka alipouona moto mbali.

9

Demane aliona jitu limeketi karibu na moto. Mkoba mkubwa ulikuwa karibu nalo. Alikaribia akichechemea kama aliyeumia mguu.

Alisema, "Naomba maji ya kunywa. Nimeumia mguu." "Nitakuletea maji lakini usiguse mkoba wangu." Jitu lilisema huku likiweka mkoba huo vizuri.

10

Jitu lilipoondoka kwenda mtoni, Demane alikata kamba ya mfuko, ukafunguka na dadake akatoka.

Demane aliubadilisha mkoba huo na wake uliojaa nyuki. Kisha yeye na dadake wakajificha na kungoja kuona kitakachotokea.

11

Jitu lilirudi na maji pamoja na watoto wake wawili, msichana na mvulana. 

Likamwambia msichana, "Kuna mlo mtamu ndani ya mkoba. Nenda ukaulete!"

Msichana alipofungua mkoba, nyuki walimwuma mkono akalia kwa sauti, "Inauma, inauma."

12

Jitu lilimwambia mvulana aende kumsaidia. Yeye pia aliumwa akalia kwa uchungu.

"Msinifanye mjinga," jitu lilisema kwa sauti huku likiufungua mkoba.

Nyuki wengi waliliuma kichwani, masikioni na machoni. Lilirukaruka na kulia kwa uchungu.

13

Jitu lilikimbia kuelekea kwenye bwawa la maji. Lilichopeka kichwa kwenye matope likakwama huko.

Liligeuka na kuwa kisiki cha mti uliokatwa. Nyuki walijenga mzinga wao kwenye kisiki hicho.

Demane na Demazane walifurahia asali tamu kutoka kwa mzinga huo.

14
You are free to download, copy, translate or adapt this story and use the illustrations as long as you attribute in the following way:
Demane na Demazane
Author - South African Folktale
Adaptation - Ursula Nafula
Illustration - Jemma Kahn
Language - Kiswahili
Level - Longer paragraphs