

Sungura alikuwa rafiki mkubwa wa Kima.
Walishiriki mambo mengi pamoja.
Siku moja Sungura alisema, "Hebu twende matembezi tukatafute chakula."
Kima alikubali bila kujua yaliyomsubiri!
Walienda katika shamba la wenyewe na kuanza kula mahindi.
Sungura alikuwa na njama ya kumtendea Kima uovu.
Sungura alimwonea Kima wivu kwa kuwa na mkia mrefu.
Alikuwa amewaeleza wenye shamba, "Kima atakuja kula mahindi yenu leo. Mfunze adabu!"
Walipokuwa wakila mahindi, Sungura alijificha na kupiga kelele akisema, "Mwizi! Mwizi! Mahindi yenu yanaliwa yote!"
Kisha akatoroka na kwenda zake. Kima hakujua kilichokuwa kikiendelea.
Ghafla, wenyewe walifika na kumpata Kima akijaribu kutoroka.
Hata hivyo, mkia wake mrefu ulimzuia kwenda haraka.
Walimfuata wakipiga kelele, "Simama! Simama! Umetumalizia mahindi yetu."
Walimshika na kuanza kumpiga.
Kima alijaribu kuponyoka na kutoroka tena lakini hakuweza.
Kima hakuweza kuvumilia kichapo. Aliwasihi waache kumchapa ili awaeleze mambo yalivyokuwa.
"Nilikuwa na rafiki yangu Sungura. Ni yeye aliyenialika," alilia.
Hata hivyo, wenyewe hawakumsikiza. Mmoja alitoa panga na kusema, "Leo ni leo! Utashika adabu!"
Aliukata mkia wake. Sungura alishuhudia kila kitu kutoka alikojificha.
Wenye shamba waliondoka na kwenda zao. Kima alipokimbilia usalama wake, Sungura aliuchukua mkia wa Kima na kwenda kuupika.
"Nitamwalika Kima kwa chakula cha mchana," alitabasamu.
Baada ya mlo, Kima alisema, "Asante rafiki yangu kwa kuandaa chakula kitamu."
Sungura alimwuliza Kima ikiwa alijua alichokuwa amekula. Bila kujua, Kima alijibu, "La, sijui!"
Sungura alisema, "Hicho kitoweo kitamu ulichokula, kilikuwa mkia wako."
Baada ya kusema hivyo, alitoroka. Na kutoka siku hiyo walikuwa maadui!

