Kiundu mlafi
Mutugi Kamundi
Alex Zablon

Hapo kale, katika kijiji cha Katumbi, aliishi mwanamme aliyeitwa Kiundu.

Alipenda sana kula nyama.

1

Mwanawe Chifu wa Katumbi alikuwa ametimu umri wa kuoa.

Chifu aliwaalika wanakijiji harusini.

2

Kiundu alipata mwaliko wa harusi hii.

Pia, alisikia kuwa kungekuwa na sherehe ya harusi katika kijiji cha Nyamani.

3

"Aaa! Sherehe mbili kwa siku moja! Lazima nihudhurie sherehe zote mbili," Kiundu aliwaza.

"Nitaenda kwanza Nyamani kisha nirudi Katumbi," akaendelea kuwaza.

4

Kiundu alirauka mapema na kuelekea Nyamani. Alipofika Nyamani, sherehe ilikuwa haijaanza.

"Nitarudi Katumbi, baadaye nirejee Nyamani," Kiundu aliamua.

5

Kiundu alirudi Katumbi. Alitarajia angekuta nyama zikiwa tayari. Baada ya safari ndefu, alihisi njaa sana.

Alipofika Katumbi, chakula kilikuwa bado hakichakuwa tayari.

6

Kiundu akawaza, "Niliwaacha wapishi Nyamani wakijiandaa kupika. Chakula lazima kiwe tayari sasa."

Kiundu aliamua kurudi Nyamani.

7

Kiundu alipofika Nyamani, watu walikuwa tayari wamekula. Wageni walikuwa wanawatuza zawadi maarusi.

Kiundu alikuwa mchoyo na hakuwa ameleta zawadi. 

Alitaka kula tu.

8

Kiundu alikasirika alipokosa chakula. Mara moja, aliamua kurudi kwao Katumbi.

Kwa vile alikuwa mwenye njaa na mchovu, hangeweza kutembea haraka.

9

Alipowasili kwao Katumbi, wageni walikuwa wamemaliza kula chakula chote. 

Walikuwa wakiimba na kucheza kwa furaha.

10

Alipoambiwa kuwa chakula kilikuwa kimeisha, Kiundu alikasirika sana.

Lo! Kiundu alizikosa nyama kwenye sherehe zote mbili.

11

Alitembea polepole akirudi nyumbani akiwa mwenye huzuni na njaa.

12
You are free to download, copy, translate or adapt this story and use the illustrations as long as you attribute in the following way:
Kiundu mlafi
Author - Mutugi Kamundi
Adaptation - Caren Echesa
Illustration - Alex Zablon
Language - Kiswahili
Level - First paragraphs