

Sisi ni waandishi chipukizi, wasanii, na wanaharakati kutoka Maktaba ya Jamii Cheche, Monduli, Tanzania.
Tuliandaa kitabu hiki kuelimisha jamii juu ya changamoto za kijinsia na kutoa mawazo yetu kuhusu namna ya kuzisuluhisha.
Baadhi ya wazazi wanawabagua watoto wa kike. Watoto wa kike wanafanyishwa kazi ngumu wakati watoto wa kiume wanasoma au kucheza.
Watoto wa kike wanaachishwa shule ili kufanyishwa kazi nzito kuliko umri wao.
Tunahitaji kuelimisha jamii kuhusu umuhimu wa watoto wa kike kwenda shuleni.
Kama mtoto anateswa nyumbani au kunyimwa haki yake ya elimu, majirani au ndugu wanaweza kumsaidia kwa kwenda naye polisi kuripoti.
Baadhi ya wasichana wanalazimishwa kuolewa wakiwa na umri mdogo na kuacha shule.
Changamoto hii inatokana na umaskini wa wazazi unaowafanya watake kupokea mahari.
Pia mtoto akifiwa na wazazi anaweza kunyimwa haki ya elimu na kuolewa mapema.
Kuolewa katika umri mdogo kunachangia kwenye ukosefu wa elimu kwa watoto wa kike na kuendelea kuongeza umaskini.
Kunasababisha watoto wa kike kushindwa kujitambua, kutokutambua haki zao, na kutokujua jinsi ya kujisaidia katika jamii.
Hatuna budi kuitisha mikutano ya kuwaelimisha watu kuhusu umuhimu wa watoto wa kike kwenda shuleni na kutokuozeshwa mapema.
Tunapoona familia ni maskini, tunatakiwa kuichangia ili wampeleke mtoto shule. Hiyo inaweza kukatisha ndoa kabla ya umri wa mtoto.
Pia tunapoona mtoto hana wazazi tunatakiwa tuombe kibali cha kumlea au kumpeleka sehemu ambapo wanalelea watoto.
Hiyo inaweza kukatisha kuolewa kabla ya wakati.
Watoto wa kiume wanakutana na changamoto ya kushawishiwa kuvuta bangi, kunywa pombe, kuiba, na kujiunga na makundi mabaya.
Mwishoni, unakuta watoto hao wameacha shule kutokana na ushawishi mitaani. Wakati mwingine, hata wasichana hukumbwa na changamoto ya kutumia bangi na pombe.
Changamoto hii inasababishwa na umaskini na kukata tamaa.
Pia inatokana na changamoto za nyumbani, kama kukosa chakula na wazazi kutokuwalea watoto katika misingi inayofaa.
Ada kubwa ya shule pia inachangia.
Tunaweza kuelimisha jamii kuhusu madhara ya uvutaji bangi kwa kupitia mitandao ya kijamii, mabango, na magazeti.
Tunahitaji kuwashawishi watu kutokujiunga na makundi yasiyofaa na kuvumilia hali ngumu waliyo nayo wazazi.
Serikali inahitaji kupunguza ada za shule na kurahihisha upatikanaji wa ajira, ili kusaidia kupunguza changamoto ya bangi.
Pia tuwasaidie watu wasikate tamaa mapema. Wazazi wajitahidi kuwalea watoto vizuri katika misingi mizuri ya maisha.
Wanawake na wasichana wanabakwa katika jamii yetu.
Polisi wanahitaji kuongeza bidii kukamata na kuwafunga wabakaji.
Mtu akibakwa anatakiwa kusema ili mhusika ashitakiwe na kukamatwa na polisi.
Ukeketaji ni changamoto katika jamii yetu.
Mtu akikeketwa, kuna uwezekano wa damu nyingi kumtoka na kusababisha kifo.
Tunahitaji kuelimisha jamii kuhusu madhara ya ukeketaji, kwa mfano kwa kupitia makongamano ya kidini.
Watoto hufanyishwa kazi ili watafute pesa ili wawatunze wazazi. Wanafanya kazi ngumu katika umri mdogo.
Hii inatokana na umasikini na changamoto za kifamilia. Mtoto mmoja hufanyishwa kazi kuliko mwingine kutokana na upendeleo wa mzazi.
Tuongee na wazazi kuwashauri wasiwafanyishe watoto kazi ngumu na wawapeleke watoto shule ili kupata elimu.
Watoto wengi wanaacha shule kwa sababu mbalimbali. Watoto wa kike wanaolewa mapema au kupewa kazi nyingi nyumbani mpaka wanaacha shule.
Watoto wa kiume wanakutana na vishawishi mtaani kama vile kuvuta bangi na kunywa pombe.
Kwa sababu ya umaskini, wazazi wanakosa ada ya shule au kushindwa kumnunulia mtoto sare za shule.
Mtoto anaingia mtaani na kufanya kazi ili kujipatia fedha za kuitunza familia.
Walimu hawafundishi vizuri na wanawachapa watoto kwa hasira.
Tutumie redio kuelimisha watu kuhusu umuhimu wa shule. Redio inaweza kutumika pia kuelimisha jamii kuhusu madhara ya uvutaji bangi.
Pia, tuelimishe jamii kuhusu umuhimu wa watoto wa kike kutokuozeshwa mapema.
Tuwaelimishe walimu kufundisha vizuri na kutokuwachapa watoto kwa hasira.
Tuwashauri afisa elimu shule zote ziwe na mahitaji yote muhimu kama maji na mazingira mazuri.
Tushauri serikali kupunguza ada za shule na tuwasaidie watu ambao hawana mahitaji ya shule.
Mtoto anaathirika na mawazo kutokana na mateso ya nyumbani.
Ugomvi baina ya wazazi humharibu mtoto kisaikolojia na mtoto anakuwa na mawazo na kushindwa kusoma vizuri darasani.
Mtoto anawaza atakula nini, atalala wapi, atapata wapi mboga za kupika, labda anateswa nyumbani na mama wa kambo.
Akiwa na msongamano wa mawazo, au hofu, hakuna kitu atakachoweza kufanya shuleni. Hii inatokana na ukosefu wa haki zake, kwa mfano chakula, mavazi, na malazi.
Tuwaelimishe wazazi wasigombane mbele ya watoto. Ugomvi wa wazazi husababisha mtoto kuwa na msongamano wa mawazo, kushindwa kusoma vizuri, na hata kuacha shule kabisa.
Tuwashirikishe walimu na afisa elimu ili wasimamie haki ya elimu.
Mzazi anampiga mtoto bila makosa. Mtoto mmoja anafanyishwa kazi kuliko mwingine kutokana na upendeleo wa mzazi. Msichana anafanya kazi nzito wakati mvulana anaangaliza TV.
Mama anamnyima mtoto asiende shuleni afanye kazi za nyumbani.
Tuelimishe jamii kuhusu ukatili wa kijinsia na tuhakikishe watoto wote wameenda shule ili wapate elimu bora, bila kuwabagua.

