Elimu Yetu
Wanafunzi wa Shule ya Msingi ya Mwasi Kaskazini
Wanafunzi wa Shule ya Msingi ya Mwasi Kaskazini

Kitabu hiki kimeandikwa na wanafunzi wa darasa la 5 wa Shule ya Msingi ya Mwasi Kaskazini.

Hawa waandishi na wachoraji wana ujuzi tofauti wa kipekee. Ujuzi huu una umuhimu wake katika jamii.

1

Naitwa Honesta Simoni Njau. Nina elimu ya upishi. Ninaweza kuandaa viungo, kuweka mafuta na chumvi kwa kiasi kwenye vyakula.

Ningependa kuwa na hoteli na kupika vyakula vitakavyohitajika na wateja.

2

Mimi ni Eliya. Nina elimu ya kutengeneza umeme. Mwalimu wangu ni babangu. Napenda kumwangalia anapotengeneza vitu kama spika na sola.

Elimu hii ni muhimu kwa sababu itaifanya Tanzania ing'are kwa mwanga wa umeme. Umeme hutusaidia kusoma usiku.

3

Ninaitwa Aleni Jakobo Njau. Nina elimu ya kucheza ngoma. Pia, ninaweza kutibu mifugo kwa kuwapa dawa, kuwadunga sindano na kuwapa chakula cha kutosha. Nilifundishwa na mamangu.

Ndoto yangu ni kuwa mchezaji ngoma maarufu, na kuwa mwanajeshi.

4

Ninaitwa Mery Emanueli Kessy. Nina elimu ya kupika. Ninaweza kupika chai, maharagwe, ndizi kwa mchuzi wa nyanya, na kukaanga mboga. Nimefundishwa na bibi yangu.

Ndoto yangu ni kuwa sista wa kumtumikia Mungu.

5

Naitwa Shedraki A. Luondo. Nina elimu ya kucheza muziki. Nilifundishwa na wazazi. Waliniambia nijiunge na wenzangu ili nicheze muziki.

Nilivyojiunga nao nikajua kucheza kama wenzangu. Ninatumaini nikiwa mkubwa nitakuwa dereva au rubani.

6

Ninaitwa Anicia Evance Lyimo. Nina elimu ya kulima. Wazazi wangu walinifundisha tukiwa shambani.

Baada ya kuona ninalima vizuri, Mama alinipa bustani ya mboga na mbegu za kupanda.

Kilimo huleta chakula, utajiri na ajira.

7

Ninaitwa Julius Trifon Njau. Nina elimu ya dini. Baba na mama wananifundisha elimu hii wanaposali na kwenda misa.

Nataka niwe padre nitembelee nchi mbalimbali kuhubiri injili. Elimu hii itasaidia watu wamjue Mungu.

8

Ninaitwa Bernadetha Alex Njau. Nina elimu ya ufugaji. Walionifundisha ni baba na mama. Elimu hii ina faida kwani inatupatia kipato na nyama.

Nikiwa mkubwa, nitafuga wanyama bila kumpoteza hata mmoja. Baadaye, nitapata mapato makubwa.

9

Ninaitwa Evagri J. Njau. Mimi nina elimu ya kucheza mpira wa miguu.

Mjomba wangu ndiye aliyenifundisha kucheza. Aliniambia, "Ili uwe mchezaji bora, ni lazima kuimarisha viungo vya mwili."

Ndoto yangu ni kuchezea timu ya Simba.

10

Ninaitwa Honorina Richadi Thomass Temba. Nina elimu ya kupika. Nilifundishwa na bibi. Elimu hii ni muhimu kwa sababu kunapokuwa na wageni ninaweza kuwapikia.

Nitakapokuwa mkubwa, nitapikia jamii inayonizunguka, kwa mfano, ikitokea sherehe kama harusi.

11

Naitwa Denisi Peteri Temba. Mimi ninapenda lugha yangu ya Kichaga.

Nina elimu ya kuchora picha na kucheza muziki. Aliyenifundisha ni baba.

Nitaboresha hivi vipaji ili vilete mapato makubwa kwangu, kwa familia na jamii.

12

Ninaitwa Julyclara Paul Temba. Nina elimu ya kukaanga samaki, chipsi, maandazi, ndizi, mihogo, nyama na kuku.

Elimu hii inawasaidia watu kuwa na afya njema, na pia, kuunganisha watu wengi. Nitaendeleza elimu hii hadi nifanye kazi kwenye hoteli kubwa.

13

Naitwa Benson Inocenti Mtui. Nina elimu ya kukamua maziwa.

Tuna ng'ombe wengi, na watu wanapenda sana maziwa yetu. Tunauza maziwa ili tupate fedha.

Nilifundishwa na bibi yangu kukamua. Aliniambia, "Ukifanya kazi kwa bidii, Mungu atakusaidia maishani."

14

Ninaitwa Alice Frank Njau. Nina elimu ya kulima. Nilifundishwa na babu na bibi. Nimejifunza kulima sehemu yenye rutuba na isiyo na majani, na kupalilia.

Nitakapokuwa mkubwa, nataka kuwa daktari bora wa mifugo na kilimo kutoka Tanzania.

15

Naitwa Epifania J. Mallya. Nina elimu ya kufuga kuku. Najua chakula wanachohitaji kuku, kiasi cha kuwapa na wakati wa kuwapa chakula.

Nataka kuwa mfugaji mashuhuri ili niweze kupata kipato kikubwa. Nitafuga kuku, mbuzi na ng'ombe.

16

Ninaitwa Eugenia Emanueli Semwali. Nina elimu ya kuimba.

Ninapenda kuimba nyimbo za Kichaga, Kiswahili, na Kiingereza.

Nyimbo hizi huwafurahisha watu.

17

Ninaitwa Leah C. Motta. Elimu yangu ni ya kulima. Kilimo kinaleta ajira na kuinua pato la taifa.

Baadhi ya shughuli za kilimo ni kuandaa shamba, kutoa magugu, kulima, kuandaa matuta, na kutengeneza vitalu.

Nitakapokuwa mkubwa, nitakuwa daktari.

18

Naitwa Catherini Alferio Njau. Nina uwezo wa kupika na kulima. Mama amenifundisha kupika. Baba alinifundisha kuotesha mboga na maua.

Kilimo hutupatia mazao, ajira na kuboresha chakula.

Ningependa kuwa mjasiriamali maarufu.

19

Ninaitwa Wilhelmi. Ninapenda sana ufugaji na mambo ya dini. Ndio maana ninapenda kuwa padri.

Elimu yangu nimepata kanisani na darasani. Katika maisha yangu, napenda kumcha Mungu na kueneza neno lake.

20

Naitwa Julitha Juliani Temba. Nina elimu ya kupika. Walionifundisha ni mama, dada, na bibi.

Ninaweza kupika ndizi, maandazi, chapati, ugali, nyama, maharagwe na wali.

Ningependa nipike hotelini na kuwafundisha wanajamii wengine upishi bora.

21

Naitwa Anicia Wiliamu Kaguo. Nina elimu ya kuuza vitu kibandani. Ninauza bidhaa kama nyanya, maandazi, chapati, mkate na samaki.

Nitakuja kuwa mfanyabiashara na kumiliki duka langu.

Ninaishi na bibi na babu. Bibi pia ni mfanyabiashara.

22

Jina langu ni Junior Alfredi Mmbo. Nina elimu ya kucheza mpira wa miguu.

Ndoto yangu ni kuwa askari au mchezaji hodari wa mpira wa miguu.

23

Ninaitwa Mariam Sadiki Joshua. Nina elimu ya kupika. Nilifundishwa elimu yangu na bibi. Napika vyakula kama uji, chai, wali, ugali na ndizi.

Tunapika ili tule tupate nguvu na kufanya kazi kwa bidii.

Vyakula vinatoka shambani. Tunaelimishwa kulima pia.

24

Jina langu ni Johnson Salum Abdul. Kipaji changu ni kucheza mpira.

Nilijifunza kucheza na wenzangu Julius, Aleni, Shedraki na Epifani uwanjani Kishimundu siku za Jumamosi.

Elimu huleta maendeleo.

25

Ninaitwa Maurini Francis Temba. Nina vipawa viwili, kuimba na kupika. Nilifundishwa na bibi kupika.

Tulipofunga shule tulienda Sanya kwa bibi. Alitufundisha kupika, kuotesha maua, kufagia, na kulisha kuku.

26

Ninaitwa Nora Aloice Temu. Kipawa changu ni kupika kama vile ugali, makande, wali, na mboga.

Pia nina elimu ya kuuza dukani bidhaa kama vile soda, mchele na maharagwe. Ninawavutia wateja wengi.

27

Ninaitwa Epifani Muga Kabila. Nina elimu ya kucheza mpira. Tangu nikiwa mdogo, nilifundishwa kucheza mpira na mjomba na kaka. Tulikuwa tunacheza mpira na jirani.

Nitaendeleza kipaji changu cha kucheza mpira. Nikiwa mkubwa ninataka kuwa rubani.

28
You are free to download, copy, translate or adapt this story and use the illustrations as long as you attribute in the following way:
Elimu Yetu
Author - Wanafunzi wa Shule ya Msingi ya Mwasi Kaskazini
Illustration - Wanafunzi wa Shule ya Msingi ya Mwasi Kaskazini
Language - Kiswahili
Level - Longer paragraphs