Mwasi Kwetu
Wanafunzi wa Shule ya Msingi ya Mwasi Kaskazini
Wanafunzi wa Shule ya Msingi ya Mwasi Kaskazini

Kitabu hiki kimeandikwa na wanafunzi wa darasa la 6 wa Shule ya Msingi Mwasi Kaskazini, kwenye mkoa wa Kilimanjaro.

Kimetokana na mijadala mipana kuhusu sifa na changamoto za jamii yetu na nafasi zetu katika kuleta mabadiliko mazuri.

1

Ninaitwa Norini. Kijiji chetu kina vyakula vya asili kama kiburu, kitawa, kitalolo na soho.

Asili yetu ni Wachaga. Tunapenda lugha yetu ya Kichaga. Ni utambulisho wetu wa asili.

Kusalimia tunasema, 'Kwamza maye' au 'Nangoto maye.'

2

Naitwa Gilbert Josephu Chacha. Jamii yetu ina Kanisa Katoliki linalopendwa na watu wengi.

Ina mto mkubwa wa Mnambe ambao watalii hupenda kuogelea ndani.

Ina majengo ya asili. Ina kima, ndege na aina nyingi za nyoka kama chatu na wosale.

3

Ninaitwa Emmanueli Honesti Temba. Kwetu watoto wote wanaenda shule.

Muda mwingine ajira hazipo kwa hiyo elimu huweza kumsaidia mtu kujiajiri mwenyewe na kuwaajiri wengine.

Sisi tunaosoma tunawashauri watoto kudadisi watu kwa kuuliza maswali.

4

Naitwa Esta Casimir Temba. Ninapenda kijiji changu kwa sababu tunashirikiana katika utawala wa mifereji, barabara na ufundi.

Kijiji chetu kina changamoto kadhaa, kama vile barabara kuporomoka.

Shuleni kwetu kuna ukosefu wa walimu na maktaba wa kujisomea.

5

Ninaitwa Braytoni Isack Ndanu. Mwasi Kaskazini tuna umeme unaotusaidia kusaga, kukoboa, kuchajisha, na kusikiliza redio. Umeme unazalishwa na maji.

Kuna mitingo inayotumika kama ngoma kwenye shughuli za jamii kama harusi na kutoa buriani.

6

Naitwa Lidya Gerald Mmbo. Ninapenda kijiji chetu kwa sababu upendo unafanya watu kuwa na umoja na amani.

Changamoto tuliyo nayo ni kukosekana kwa barabara. Mvua zikinyesha, magari hayawezi kupita hivyo inabidi tuweke moramu. Bila moramu ajali zitatokea.

7

Ninaitwa Magreth Kristofa Mangale. Kijiji chetu kina kanisa linalosaidia watu kusali na kumwomba Mungu kwa makini.

Zamani watu walikuwa wanatembea mpaka kwenye Mlima Kilimanjaro na kwenda kazini ili Mungu afanikishe kazi za mikono yao.

8

Ninaitwa Marck Erik Temba. Jamii yetu ina mazao mengi. Kuna ndizi, maparachichi, maembe na mbogamboga. Ardhi yetu ina rutuba.

Jamii yetu inafuga mifugo kama ng'ombe, mbuzi na kuku. Ni vyakula kwetu. Pia watu huwauza wanyama na kupata fedha.

9

Ninaitwa Esta Mendadi Temba. Kijiji cha Mwasi kina miti ya matunda inayotupatia afya bora.

Kuna vyakula vya asili kama ndizi za mbala, soho, kiburu. Sisi hupendelea vyakula hivyo sana. Kokora maye!

10

Ninaitwa Cathbert Joseph Njau. Kijiji chetu kina kanisa kubwa na nzuri. Wananchi walishirikiana kulijenga.

Pia kina mifugo wengi.

Changamoto ni ukosefu wa hospitali na zahanati. Mgonjwa afikapo hospitali jirani, unakuta ameshazidiwa.

11

Ninaitwa Maurini Frank Njau. Kijiji cha Mwasi kina shule. Wanafunzi wa Mwasi ni wasikivu, watiifu na wana nidhamu.

Changamoto ni vijana wa Mwasi wanajishughulisha na ulevi. Ninawashauri wasiwe walevi. Ulevi unasababisha madhara ya mwili.

12

Ninaitwa Bensoni Fredi Njau. Kijiji chetu kimebarikiwa na amani na uelewano. Kimebarikiwa na vitu vingi kama mifugo, vyakula, matunda na vyumba vya asili.

Kijiji chetu kina uhaba wa walimu wa kufundisha na mapadre wa kuhubiri dini.

13

Mimi ninaitwa Sofia Florian Mushi. Kijiji chetu kina sifa ya maji. Pia kina upendo. Wageni wakija kijijini kwetu tunawakaribisha kwa upendo mkubwa sana.

Changamoto ni kwamba ulevi umezidi sana. Tunajitahidi sana kuepuka tabia ya ulevi.

14

Ninaitwa Brighton Felix Temba. Mwasi Kaskazini kuna ushirikiano unaotokea pale mtu anapofiwa, wanakijiji wanamchangia.

Tulishirikiana kuchimba mfereji wa kuanzia Ngoma na kuishia Mamboleo. Tuna changamoto ya kukosa maktaba.

15

Ninaitwa Robisoni Raimondi Njau. Kijijini kwetu kuna rasilimali ya maji. Kuna ardhi yenye rutuba.

Tumebarikiwa na wachapakazi wengi.

Kuna changamoto ya wezi wanaoiba kuku, mbuzi na ndizi.

16

Katika kijiji chetu tunashirikiana kuchimba visima vya maji na kuboresha mabomba ya maji na visima.

Kuna vyakula vya asili kama mbande, ndizi na soho.

Kuna changamoto ya watu kulewa sana na kuanza matusi.

17

Ninaitwa Chirispin Joseph Materu. Mwasi kwetu tunatumia pikipiki, bajaji na magari kusafirisha watu na mizigo.

Kuna changamoto ya usafi wa mazingira.

18

Ninaitwa Clemensi Hilimerdi Njau. Tunafurahia sana kuwa na maji ya kutosha.

Wengine wanachafua mifereji kwa kukojoa hapo na kuchafua kwa kutupa taka ovyo.

19

Ninaitwa Ovino Gaspari Temba.

Kijiji chetu kinajivunia kuwa na wachapakazi wengi wanaoshirikiana katika kazi za jamii.

20

Naitwa Glory Prosper Ngowi. Tuna shule nyingi katika jamii yetu. Zamani hatukuwa na shule. Tunapenda kusikiliza wanachotufundisha walimu.

Tunakuwa na changamoto wakati mabomba yanakauka na kutulazimisha kwenda mbali kuchota maji.

21

Ninaitwa Emmanueli Antoni Lyimo. Kijijini kwetu watu wengi hupenda kuongea Kichaga. Tunapenda lugha yetu.

Kuna changamoto ya uwizi wa mazao. Watu waliootesha wanaanza kukata tamaa ya kuendelea kufanya kazi yao.

22

Ninaitwa Evansi Danieli Lyimo. Mwasi kwetu watu hufanya kazi bila uvivu na kwa ushirikiano mzuri. Tunapendana na majirani wanaotuzunguka katika jamii.

Kuna ukosefu wa nyumba na kuna watu maskini ambao hawana nguvu, viatu, na nyumba.

23

Ninaitwa Glory Gasper Lugwisha. Kijiji chetu kina wakulima, wa mahindi, maharagwe, mihogo na mpunga.

Tuna changamoto ya wizi.

24

Ninaitwa Eladius Florian Temba. Zamani shule iliyokuwepo ilianzia darasa la 1 hadi la 4. Ukifaulu Waingereza wanakusomesha zaidi. Kulikuwa na Middle School kwa watu wenye fedha.

Sasa kijijini kwetu kuna shule nyingi na watoto wote husoma.

25

Ninaitwa Dismas Liberati Temba. Mwasi kwetu watu wanafuga bata, mbuzi, ng'ombe, kondoo, kuku na kanga.

Hata mimi ninafuga sungura.

Kuna changamoto ya wizi. Wtu wanaiba hadi nguo kwenye kamba. Ukifua nguo hautaondoka nyumbani hadi zikauke.

26

Kwa majina naitwa Brighton Gerald Mmbo. Rasilimali zinazopatikana Mwasi ni maji, mifugo, mabonde, mito na milima.

Umoja na ushirikiano unapatikana katika misiba, sherehe, mavuno na kilimo.

Changamoto ni ukosefu wa vitabu vya kujisomea.

27
You are free to download, copy, translate or adapt this story and use the illustrations as long as you attribute in the following way:
Mwasi Kwetu
Author - Wanafunzi wa Shule ya Msingi ya Mwasi Kaskazini
Illustration - Wanafunzi wa Shule ya Msingi ya Mwasi Kaskazini
Language - Kiswahili
Level - Longer paragraphs