

Katika eneo la Sirani paliishi familia ya watu wanne.
Baba, Mama na mapacha wao wawili, Baraka na Njoroge.
Familia hiyo iliishi kwa amani na upendo. Walishirikiana kufanya kazi.
Baba na mapacha walilima shambani. Mama naye alifanya usafi wa nyumba na kuchota maji.
Siku moja Mama yao aliwaita Baraka na Njoroge awatume dukani kununua sukari.
Bila kupoteza muda walielekea dukani.
Walinunua sukari na kuanza kurudi nyumbani.
Walitumia njia ya mkato inayopita kwenye vichaka ili waweze kufika nyumbani kwa haraka.
Walipofika katikati, walimwona kifaru akija. Walipatwa na hofu kubwa.
Baraka alimwambia Njoroge apande juu ya mti. Naye alilala chini na kutulia kama maiti.
Walitetemeka sana.
Kifaru alipomwona Baraka amelala, alimnusa nusa. Akidhani kuwa si hai, alienda zake kichakani.
Hakumuona Njoroge aliyekuwa juu ya mti.
Njoroge alishuka kutoka mtini bado akiwa na hofu. Walichungulia alipokuwa ameenda yule kifaru lakini hawakumuona.
Walitimua mbio hadi nyumbani.
Mara tu walipofika nyumbani walisimulia wazazi wao kitendo hicho.
Waliapa ya kwamba hawatawahi kupitia njia za mkato tena.

