Ndugu mapacha
Abigel Kaari
Abigel Kaari

Katika eneo la Sirani paliishi familia ya watu wanne.

Baba, Mama na mapacha wao wawili, Baraka na Njoroge.

1

Familia hiyo iliishi kwa amani na upendo. Walishirikiana kufanya kazi.

Baba na mapacha walilima shambani. Mama naye alifanya usafi wa nyumba na kuchota maji.

2

Siku moja Mama yao aliwaita Baraka na Njoroge awatume dukani kununua sukari.

Bila kupoteza muda walielekea dukani.

3

Walinunua sukari na kuanza kurudi nyumbani.

Walitumia njia ya mkato inayopita kwenye vichaka ili waweze kufika nyumbani kwa haraka.

4

Walipofika katikati, walimwona kifaru akija. Walipatwa na hofu kubwa.

Baraka alimwambia Njoroge apande juu ya mti. Naye alilala chini na kutulia kama maiti.

Walitetemeka sana.

5

Kifaru alipomwona Baraka amelala, alimnusa nusa. Akidhani kuwa si hai, alienda zake kichakani.

Hakumuona Njoroge aliyekuwa juu ya mti.

6

Njoroge alishuka kutoka mtini bado akiwa na hofu. Walichungulia alipokuwa ameenda yule kifaru lakini hawakumuona.

Walitimua mbio hadi nyumbani.

7

Mara tu walipofika nyumbani walisimulia wazazi wao kitendo hicho.

Waliapa ya kwamba hawatawahi kupitia njia za mkato tena.

8
You are free to download, copy, translate or adapt this story and use the illustrations as long as you attribute in the following way:
Ndugu mapacha
Author - Abigel Kaari
Illustration - Abigel Kaari
Language - Kiswahili
Level - First paragraphs