Urafiki kati ya Paka na Panya
Hildah mukiri
Bradon karani

Paka na Panya waliishi katika kisiwa kimoja. Walipendana sana. Paka alichoka kuishi kisiwani na kumwambia Panya kuwa angetaka kuenda ng'ambo.

Panya alifurahishwa na wazo hilo akaamua kumfuata. Papo hapo wakaamua kutengeneza mtumbwi.

1

Wakachukua gogo kubwa na kuchimba ndani.

Gogo likawa kama mashua kisha wakalitia majini likaelea.

2

Siku iliyofuata, walianza safari yao asubuhi na mapema. Waliabiri kwenye gogo walilotengeza.

Ilipofika jioni, Paka alihisi njaa na kumwambia Panya kuwa atamla.

"Tazama nilivyokonda. Hutashiba ukinila," Panya akasema.

3

Panya alianza kutafuna gogo lao walilokuwa wakisafiria.

Paka alipoamka alishangaa kumuona Panya akila. Paka akamwuliza, "Unakula nini?"

4

Panya akamjibu rafikiye Paka, "Tutakufa njaa. Tule mashua yetu!"

Paka alijaribu kula gogo lakini hakupenda ladha yake.

Panya aliendelea kulila gogo mpaka mtubwi wao ukatoboka.

5

Wakaanza kuzama. Panya aliruka majini akaogelea vizuri lakini Paka alipata shida kubwa majini.

Baada ya Panya kumsaidia, alitoka salama salimini na kwa bahati, wakafika ng'ambo.

6

Paka alikuwa na njaa sana. Akamwambia Panya, "Sasa nitakukula maana umenona sana. Sikuachi!"

Panya alishangaa kwa muda kisha akasema, "Sawa, nimekubali utanila lakini nina matope mikononi. Subiri ninawe kwanza."

7

Panya aliingia kwenye shimo chini ya mti. Paka alimngoja nje lakini Panya hakutokea tena.

Hadi leo, Paka anapoliona shimo popote, hungojea pale ili amle Panya.

8
You are free to download, copy, translate or adapt this story and use the illustrations as long as you attribute in the following way:
Urafiki kati ya Paka na Panya
Author - Hildah mukiri
Illustration - Bradon karani
Language - Kiswahili
Level - Longer paragraphs