

Juma alikuwa mwanafunzi wa shule ya msingi ya Katoloni. Aliishi na babake Musa.
Kila wakati babake angemwamsha mapema ili ajitayarishe kwenda shule.
Alipokuwa akijitayarisha kwenda shuleni, naye babake aliyekuwa na ujuzi wa kupika, angemwandalia kifungua kinywa.
Kila alipofiikiria chakula cha babake, alitabasamu.
Siku moja, alitoka shuleni akihisi njaa sana. Alienda jikoni na kumwuliza babake kama kulikuwa na chakula chochote.
Babake alimpakulia wali aliokuwa amepika.
Juma alipenda kula lakini hakupenda kupika. Baada ya babake kumpakulia wali, alimuongezea supu.
Alitabasamu kwa chakula alichokipenda.
Alipokionja, akagundua hakikuwa na ladha ambayo aliizoea.
Alishangaa kwa sababu baba yake alikuwa mpishi hodari.
Juma hakuelewa ni nini chakula kilikosa wala hakufahamu viungo vyovyote vilivyotumika kwa mapishi.
Yeye hakutaka kujihusisha na mambo ya jikoni ya upishi ila tu alifurahia chakula kitamu.
Alimwita babake na kumjulisha kuwa chakula hakikuwa na ladha. Babake aliamua kuendea mkebe wa chumvi na kuimwaga kwenye chakula kisha akakoroga.
Juma hakuelewa kiwango cha chumvi kinachostahili kuwekwa kwenye chakula kwa kuwa hakupenda upishi.
Mara tu alipokionja, ulimi wake uliwasha, alikodoa macho huku pua ikikunjika. Hakujua amwite nani wala aguse wapi.
Uzembe na ulafi wake ulimtia matatani. Alilia kwa uchungu huku akipanguza ulimi kutumia meza.
Babake aliangua kicheko. Juma aliona haya huku tumbo likinguruma.
Tangu siku hiyo, Juma aliamua kujifunza upishi na kufanya kazi za jikoni. Babake alifurahi kwa kuwa Juma alipata funzo lake.

