

Hapo zamani, kulikuwa na mamba mwenye njaa aliyeishi mtoni. Aliwakamata wanyama kama mbuzi, ng'ombe na kondoo walipokwenda kunywa maji.
Wanyama wote wakaisha. Wakabaki ndege na mbuni. Mamba hakuweza kuwakamata ndege kwa vile wanaruka.
Siku moja, mamba alihisi njaa sana na alikuwa amewamaliza wanyama wote. Siku hiyo mbuni alikuwa anaelekea mtoni kunywa maji.
Mamba akamwambia, "Mbuni, naomba uje uniangalie jino langu. Linauma sana."
Mbuni alikwenda kwa mbuni kumuangalia jino lake.
Mbuni akaingiza kichwa chake ndani ya mdomo wa mamba kuangalia jino la mamba lililokuwa likiuma.
Mbuni akamwuliza mamba, "Jino lipi?"
Mamba akamwambia, "La chini, upande wa kulia."
Mara mamba akafunga mdomo wake.
Mbuni akaanza kujivuta. Akajivuta, akajivuta! Hakufanikiwa kujitoa. Shingo yake ikaanza kuwa ndefu sana.
Mamba naye, hakuweza kufunga mdomo wake sana. Akamuachilia mbuni.
Mbuni akaondoka na kuelekea nyumbani kwake.
Na ndio maana hadi leo mbuni ana shingo ndefu.

