

Mimi ninaitwa Noeli. Nina miaka tisa. Nasoma darasa la pili.
Kipaji changu ni kuwa mwanajeshi. Nitalinda nchi yetu ili isiingiliwe na jambazi.
Ninaitwa Josephina John. Ninasoma darasa la nne. Nina miaka kumi.
Kipaji changu ni kuchora. Mimi ninapenda kuchora sana. Ninachora vitu mbalimbali kama vile dawati, mtu, na maua.
Mimi ninaitwa Merry Beatus Maiko. Ninasoma darasa la nne katika Shule ya Msingi Sinoni. Katika familia yetu tupo watu wanne.
Ninadhania nitakapokuwa mkubwa nitakuwa mwanasayansi. Kwa sasa kipaji changu ni kucheza mpira wa miguu.
Kwa majina naitwa Juniour Daudi. Nina kipaji cha kucheza mpira wa miguu. Nilipokuwa mdogo, nilikuwa natamani kucheza mpira wa miguu.
Nilijifunza kucheza mpira huo nikiwa shuleni. Kila siku ya Ijumaa shuleni tulikuwa tukienda kwenye uwanja wa polisi tulikofanyia mazoezi.
Siku moja, nilicheza mpira wa miguu nikachaguliwa kuichezea timu ya shule.
Pia nina kipaji cha kuchora. Ninapenda kuchora na kucheza mpira wa miguu. Ninapenda hivyo vipaji vyote.
Kwa majina naitwa Lulu Hassani Issa Feruzi. Nasoma Shule ya Msingi Ngarash. Niko darasa la nne na nina miaka kumi na mmoja.
Nakaa Tanga na kabila langu ni la Kizengua. Napenda chakula cha Kizengua kiitwacho goge.
Kipaji changu ni kuandika shairi.
Ndoto yangu ni kuwa mwandishi wa mashairi yatakayochapishwa kwenye vitabu vya Maktaba ya Jamii Cheche.
Mimi ninaitwa Caren Emanuel. Ninasoma darasa la pili katika Shule ya Msingi Ngarash.
Kipaji changu ni kuwa mwalimu. Ningependa kufundisha Shule ya Mlimani nitakapomaliza shule.
Kwa majina ninaitwa Kelvin Peter. Ninasoma darasa la saba katika Shule ya Msingi Mazoezi.
Kipaji changu ni kuchora. Ninapenda sana kuchora. Nilipofikia miaka 7 nilianza kujua kipaji changu nikawa ninakiendeleza.
Hadi sasa ninapenda kuchora.
Sio kuchora tu bali nina kipaji kingine kama vile kucheza mpira, kusoma na kuandika.
Ningependa sana kuwahimiza kuwa mkiviendeleza vipaji vyenu bila kuwa waoga, mtaweza kupata ajira.
Kuhusu vipaji vya wengine, ninapenda sana kusikia mtu akiendeleza kipaji chake.
Changamoto ninazozipata ni kukosa vifaa vya kuchorea kama vile karatasi nyeupe na penseli, na rangi za aina mbalimbali.
Kwa majina ninaitwa Kelvini Zubery Akaro. Nilipoanzishwa chekechea nilichekwa na wenzangu kwamba mimi sina sauti ya uimbaji. Nililia sana.
Nikakutana na rafiki yangu aliyeitwa Kelvini Peter. Alinishauri nisikate tamaa.
Pamoja, tulishirikiana kukuza vipaji vyetu. Tulisoma vizuri tulipokuwa chekechea na tulipata nafasi katika Shule ya Msingi Mazoezi. Nilisoma kwa bidii.
Haikuwa rahisi kupata nafasi ya kujisomea na kufanyia kipaji changu mazoezi.
Nilikuwa nikijifungia ndani na kujifunza kuimba. Nilijaribu kuchora, lakini ilikuwa vigumu pia.
Ghafla, nilipata habari kuwa kuna kipindi cha mapishi kila tatu usiku.
Nilifuatilia kwa makini sana. Hivi sasa nina vipaji vya uimbaji, uchoraji na upishi.
Naitwa Angel Dismas Peter. Ninasoma darasa la nne katika Shule ya Msingi Ngarash.
Nina kipaji cha kuwa mwanasayansi. Katika familia yetu tuko tisa. Napenda kufaulu katika kipaji changu. Najitahidi kusoma sayansi ili niweze kufanyia kazi kipaji changu.
Kwa jina ninaitwa Gladinesi Samsoni. Ninasoma darasa la nne. Ninasoma Shule ya Mazoezi.
Kabila langu ni Mmeru. Chakula chetu ni kiburu. Ni chakula ninachokipenda sana.
Kipaji changu ni kutunga mashairi. Nitakiendeleza.
Ninatarajia kuwa mtungaji wa mashairi na kujulikana kitaifa na katika nchi za nje.
Ningependa kuwa kama watunzi mashairi wengine wakubwa na kufikia malengo yangu.
Ninapenda kipaji changu.
Kwa majina ninaitwa Doto. Nina kipaji cha kucheza mpira na kuchora. Mimi ni mchezaji mzuri na ninapenda kucheza mpira sana.
Pia mimi ni mchoraji mzuri sana na ninapenda kuchora watu wanaocheza mpira wa miguu.
Mimi naitwa Meshack Daudi. Nina umri wa miaka sita. Ninasoma darasa la kwanza Shule ya Msingi Ngarash.
Kipaji changu ni kucheza mpira. Ninapenda kipaji changu na ninataka nikiendeleze.
Kwa majina ninaitwa Honnoratha Innocent Akaro. Nasoma Shule ya Msingi Mazoezi. Niko darasa la nne. Nina miaka tisa.
Mimi ni Mchaga wa Materuni, mkoa wa Kilimanjaro.
Napenda chakula cha Kichaga kiitwacho kiburu.
Kipaji changu ni sayansi na teknolojia. Ndoto zangu ni kuja kuwa daktari wa upasuaji, katika hospitali ya KCMC, wilayani Moshi, mkoa wa Kilimanjaro.
Nimejiwekea malengo ya kufanya kazi ya udaktari.
Baada ya kuajiriwa, nitawajengea wazazi wangu nyumba na kuinunulia familia gari. Baada ya hapo, nitajinunulia nyumba na gari.
Hii picha inaelezea kwamba kibakuli, penseli na maji ni mahitaji muhimu katika hatua ninazochukwa.
Naitwa Burai Balitazari Mrema. Nina miaka 8. Ninasoma darasa la pili.
Kipaji changu ni kucheza mpira wa miguu. Mimi ni mchezaji wa timu ya Yanga. Ninacheza mbele na kudaka.
Naitwa Benson Maiko Laitery. Ninasoma darasa la sita Shule ya Msingi Ngarash. Nina miaka 12.
Kipaji changu ni kucheza mpira wa miguu. Ninapenda kucheza mpira kwa sababu hufurahisha mwili na pia hunufaisha akili.
Nilipokuwa darasa la tano, nilitamani kucheza sana kwenye timu ya shule. Siku moja nilichaguliwa kuchezea timu ya shule. Hadi sasa ninaendelea kucheza.
Hata nikiwa mkubwa ninataka kuwa mchezaji wa Timu ya Taifa Tanzania. Hili ni ombi langu kwa Mungu.
Mimi naitwa Matiasi Zuberi. Ninasoma darasa la kwanza.
Kipaji changu ni sayansi. Nataka niwe daktari niwahudumie watu.
Pia nina kipaji cha kufuga ng'ombe. Najua kuwachunga ng'ombe na ningependa kuwahudumia wanyama pia.
Mimi ninaitwa Alidi Paulo. Ninasoma darasa la tatu.
Ninataka kuwa mwalimu niwafundishe wanafunzi. Kipaji changu ni kuwafundisha wanafunzi na kuwaletea vitabu.
Kwa majina ninaitwa Wenworth Maurice Mwita. Nina miaka saba. Ninasoma darasa la pili katika Shule ya Msingi Penieli.
Kipaji changu ni kuwa dereva. Nikiwa mkubwa nataka kuwa dereva na kusomea mambo ya utalii.
Kwa majina naitwa Marvin Loth Edward. Ninasoma darasa la tano Shule ya Msingi Sinoni. Nina miaka kumi na moja.
Kipaji changu ni kucheza mpira wa miguu na kuchora. Hata sasa mimi ninaendelea kukuza vipaji vyangu.

