

Mzee Nyembe alikuwa akiishi na familia yake kijijini.
Familia hiyo ilijaa ufukara.
Mzee Nyembe alijitahidi sana kwenye shughuli zake za uwindaji.
Lakini, hakufanikiwa.
Mzee Nyembe akampa moyo mke wake ili asikate tamaa.
Kisha, akamwaga na kuelekea porini yalipokuwa mawindo yake.
Mzee Nyembe alitembea msituni kukagua mitego yake.
Hakuamini kwani mtego mmoja ulikuwa umemnasa twiga.
Mzee Nyembe hakuweza kuamini macho yake!
Akajiwazia mwenyewe na kusema, "Sasa, umasikini umeniishia. Twiga huyu atanipa faida kubwa sana."
Twiga akiwa pale naye akasema, "Tafadhali bwana wangu, kama hutojali nataka kukuonyesha utajiri."
Mzee Nyembe akashangaa kusikia kuwa twiga huyo angeweza kumuonyesha utajiri.
Akamwuuliza, "Wapi ulipo utajiri? Ukinionyesha nitakuacha huru uende zako."
Twiga akajibu, "Utajiri huo upo mwilini mwangu. Unajua kwa nini niliumbwa mrefu kuliko wanyama wote?"
Mzee Nyembe akajibu, "Hapana! Sijui!"
Twiga akaendelea, "Ni kwa sababu kichwani mwangu vipo vipande vya dhahabu."
Mzee Nyembe alistaajabu kusikia habari hiyo.
Twiga akaendelea, "Unajua jinsi unaweza kuvipata hivyo vipande vya dhahabu?"
Mzee Nyembe akajibu, "Sijui! Tafadhali, nieleze nijue."
Twiga akasema, "Ukinifungua, nitakuonyesha jinsi ya kupata hivyo vipande vya dhahabu."
Mzee Nyembe akapatwa na tamaa.
Alikuwa na tamaa kubwa ya kupata vipande vya dhahabu.
Akafanya haraka kumfungua twiga kutoka mtegoni.
Twiga huyo alipofunguliwa, alimpiga teke mzee Nyembe akaanguka chini.
Mzee Nyembe alijitahidi kumkamta twiga, lakini alishindwa.
Mzee Nyembe akarudi nyumbani akiwa na upweke mkubwa kwa kumkosa twiga.

