

Mara hii familia yangu iliamua kuzuru mji wa Kisumu na kuliona ziwa la Victoria.
Kutoka mji mkuu wa Nairobi mpaka Kisumu ni kama kilomita 425 kwa gari.
Ziwa la Victoria linamilikiwa na nchi tatu: Kenya, Uganda na Tanzania.
Ziwa hili limezingirwa na Bonde Kuu la Ufa.
Kuna samaki wengi, kwa hivyo, tuliweza kuwaona wanawake na wanaume wakivua samaki.
Wanawake waliingia majini na kuvua kwa kuwatega kwa mitego midogo.
Wanawake hutumia mitego kama hii na kuwashika samaki wengi wadogo.
Huwapika samaki hao na kulisha jamii zao.
Wanaume hutumia mashua kuvua.
Kwa hivyo, huweza kuwavua samaki wakubwa kuliko kina mama.
Tuliwaona wavuvi wakiwaleta samaki ukingoni mwa ziwa.
Samaki mkubwa ambaye hupatikana katika ziwa hili ni mbuta.
Tuliyemwona alikuwa na uzito wa kilo 140 na urefu wa mita 1.8.
Pia tuliweza kupata wanyama kama mamba na kiboko.
Hawa wanyama wawili ni hatari sana kwa maisha ya watu. Watu kiasi hupoteza maisha yao wanaposhambuliwa.
Hivi karibuni ziwa limevamiwa na gugu linaloenea na kufunika maji.
Wataalamu wanajaribu kutatua janga hili.
Ziwa hili ni muhimu kwa nchi nyingi kwani ndio mwanzo wa mto mrefu zaidi duniani.
Mto wa Nile umeanza katika ziwa hili na kwenda mpaka Misri. Niliweza kwenda mahali mto huu unapoanzia.
Baadaye, tuliwauliza wenyeji pahali pazuri pa kupata lishe. Tuliekezwa kwenye Hoteli Kiboko iliyoko ukingoni mwa ziwa.
Tulikula samaki wa kukaangwa, ugali, sukuma wiki, kachumbari na biriani. Tamu sana!
Hata kama nilihuzunika kuona ziwa lilivyoharibiwa na gugu, nilifurahia safari yangu.
Zoezi
1. Kutoka Nairobi mpaka Ziwa la Victoria ni kilomita ngapi?
2. Ziwa la Victoria linamilikiwa na nchi tatu: _________, ________ na ___________.
3.Ni samaki gani mkubwa anayepatikana katika ziwa hili?
4. Ni mto gani maarufu duniani unaoanza kutoka hapa?
5. Ni Wanyama gani hatari wanaopatikana hapa?

