Safari ya Mombasa
Njeri Wachira

Tulisafiri kwa treni ya SGR kutoka mji mkuu wa Nairobi kuelekea mji wa Mombasa.

1

Ndani ya treni tuliweza kununua chai na vitafunio.

Usafi wa treni ulikuwa wa hali ya juu na huduma kwa wateja ilipendeza.

2

Njiani tuliona miji midogo midogo treni iliposimama kupokea abiria na kuwashusha wengine.

Niliona miji kama Voi na Mtito Andei.

3

Tulipofika Mombasa, tulishuka kutoka kwenye treni na kupokea mizigo yetu.

Nilipigwa na mshangao kwani kulikuwa na joto jingi sana. Nilianza kutokwa na jasho ingawa kulikuwa jioni.

Tulielewa kuwa tungetumia tuktuk kwenda hadi kwenye hoteli.

4

Ndani ya hoteli tulijiburudisha kwa madafu baridi.

Pepep zote zilifunguliwa ili kupata nafuu kotokana na joto.

5

Asubuhi iliyofuata, tulienda kuiona Bahari ya Hindi.

Tulienda upande wa ufuko wa Serena. Mchanga wake mweupe ulipendeza sana.

6

Tuliogelea kwenye maji yaliyokuwa na joto kiasi na kutembea mchangani. Wachuuzi wa bidhaa mbalimbali walituzingira wakitaka tununue.

Tuliamua kulipa mashua moja itupeleke ndani kidogo.

7

Tulienda kuwaona samaki wa baharini. Vijana walioongoza mashua walimwaga chakula majini kuwalisha samaki.

Samaki wa rangi ya nili, rangi ya chungwa, wa manjano na nyeusi walitokea kula.

Tulichangamka kweli kweli!

8

Mashua ilitia nanga juu ya kisiwa kimoja kidogo sana.

Hapo tulimwona pweza tukamshika na kupigwa picha naye.

9

Tulipewa vifaa mbali mbali vya kuvaa halafu tukaingia majini kuogelea na samaki aina nyinyi wenye rangi tofauti.

Nilijaribu kuwashika, lakini waliponyoka kila nilipofikiri nimefaulu.

10

Siku iliyofuata, tulienda kuiona Ngome ya Kristo iliyojengwa mwaka wa 1593.

11

Ndani ya ngome, tuliviona vitu vingi vya zamani kama ngoma, vichana, mashua na silaha za vita.

12

Katika Mji wa Kale, tuliona milango spesheli iliyoundwa kwa ustadi.

Pia, tuliona barabara za zamani zilizokuwa nyembamba kupindukia.

13

Mombasa kuna joto jingi, kwa hivyo, mavazi ya mwafaka ni mepesi na ya kulegea.

Mama yangu alinunua vazi liitwalo dera. Naye baba akanunua kanzu.

14

Minazi ilikua kwa wingi na nazi ziliuzwa kila pahali.

Tulinunua nazi nyingi pamoja na madafu na vibanzi vya muhogo.

15

Baadaye, tulijiburudisha kwa soda za aina tofauti na tukala biriani kwa mchuzi wa mbuzi.

16
You are free to download, copy, translate or adapt this story and use the illustrations as long as you attribute in the following way:
Safari ya Mombasa
Author - Njeri Wachira
Illustration -
Language - Kiswahili
Level - Longer paragraphs