

Kosi na Farida ni marafiki. Wao wanapendana sana na wote wawili wanasoma shule ya Fariji. Kosi na Farida si marafiki tu bali ni majirani.
Farida anapenda masomo sana na huwa anaamka mapema kufanya marudio. Kila anapoamka, huwa anamwamsha Kosi.
Kosi huchukua wakati sana kabla ya kuamka. Yeye ni mvivu sana.
Baada ya kusoma wanajitayarisha na kuenda shule pamoja.
Farida hufanya kazi kwao baada ya shule. Kosi hupenda tu kula kila wakati na kucheza bila kufanya kazi.
Wazazi humuonya Kosi kuacha tabia hiyo, lakini huwa hasikii. Wao humshauri aige tabia za rafiki yake Farida.
Wakati wa likizo, Farida alikuwa akiwafuata wazazi wake shambani kila siku. Alitaka kujifunza mambo mapya wakati huo wa likizo.
Farida alipokuwa akimwambia Kosi waende shambani, Kosi alisema kuwa alikuwa amechoka sana. Au alisema kuwa alikuwa akiumwa sana na kichwa.
Kosi angeonekana tu kwa kina Farida wakati wa kula. Tabia hii ilimfanya Farida kuhisi vibaya.
Farida alipata wazo la kumsaidia rafiki yake kuacha uvivu. Aliamua watengeneze bustani ya maua na kufuga mbwa.
Baada ya kumwambia, Kosi alifurahishwa sana na wazo hilo. Wazazi wao pia waliwasaidia kutayarisha bustani ile. Vilevile, waliwapa pesa za kununua mbwa.
Baada ya siku kadhaa, maua yao yalianza kumea vizuri. Maua ya Kosi yalihitaji maji.
Kila mtu alitamani kuwa na maua kama yale. Farida na Kosi waliendelea kutia bidii kufanya bustani ipendeze zaidi.
Kila asubuhi Kosi alipaswa kunyunyizia maua maji naye Farida kuwalisha mbwa.
Kosi alizidisha bidii kabisa Jambo ambalo lilifanya wazazi wake kustaajabu.
Alianza kuamka mapema bila kuambiwa na mtu. Hakupata wakati wa kulala mchana.
Wakati mwingine alisahau kula chakula na kukumbushwa na mamake.
Alifurahia sana na kumshukuru rafiki yake Farida.

