

Hapo zamani, kulikuwa na marafiki wawili, Kinywa na Mkono.
Waliishi kijijini kama ndugu kila mmoja na mkewe.
Baada ya muda mfupi, mke wa Kinywa alifariki.
Kinywa alimwomba rafiki yake vifaa ili amzike mke wake.
Kinywa aliporudi nyumbani, aligundua kwamba alikuwa amelipoteza panga la Mkono. Alienda kuomba msamaha ila Mkono hakutaka kusikia maelezo yoyote.
Mkono alimlazimisha Kinywa amrudishie panga lake na lisiwe jingine bali lile alilokuwa amemuazima.
Kinywa hakuwa na la kufanya. Aliamua kurudi alipomzika mkewe ili alitafute panga hilo. Alitafuta kila mahali lakini, hakulipata.
Mwishowe, aliamua kuchimbua kaburi ili angalie. La kushangaza ni kuwa hata mwili wa mkewe haukuwepo tena kaburini.
Kwa huzuni, Kinywa alirudi nyumbani. Alipokaribia kufika, alimwona mbwa akiwa na panga hilo. Wakati huo, aliisikia sauti ya mkewe ikisema, "Huyu ni mtumishi wako."
Kinywa alilichukua panga lile akamrudishia Mkono. Yeye akabaki na mbwa yule.
Kinywa aliishi na mbwa yule akimsaidia kuwinda. Siku moja aliacha kumwita mbwa na kuanza kumwita Mtumishi.
Waliishi kwa furaha hadi urafiki baina ya Kinywa na Mkono uliporudi kuwa kama ulivyokuwa mbeleni.
Baadaye, Mkono alitamani kula nyama, lakini hakuwa na mbwa wa kumwindia. Alikwenda kuomba mbwa wa Kinywa.
Kinywa hakusita kumpatia Mtumishi wake. Lakini alimwambia asimwite mbwa bali amwite Mtumishi.
Mkono alienda na Mtumishi popote alipotaka. Kila alichomtaka afanye, alifanya.
Allimtuma porini kuwinda. Mkono alimfurahia Mtumishi sana.
Siku moja walipokuwa porini, Mtumishi alipotea. Kinywa alianza kumwita, "Mtumishi! Mtumishi! Uko wapi?"
Alipochoka, alisema kwa hasira, "Mbwa huyu ni gaidi sana." Wakati huo Mtumishi alitokea na kusema, "Umeniita mbwa! Naenda zangu." Alitoroka.
Mkono alirudi nyumbani bila Mtumishi. Alienda kwa rafikiye Kinywa kumpasha habari ya kupotea kwa Mtumishi. Kinywa hakufurahia ujumbe huo.
Alimlazimisha Mkono kumrudishia Mtumishi wake. Mkono hakufaulu kufanya hivyo.
Tangu siku hiyo hadi leo, mkono ni mtumishi wa kinywa.

