

Hapo zamani za kale, palikuwa na mfalme.
Yeye na wake zake watatu, waliishi katika kijiji kimoja kilichoitwa Nuru.
Siku moja, mfalme yule aliwaita wake zake na kusema, "Wake zangu wapendwa, ningependa leo nile chakula kitamu. Atakayepika chakula kitamu zaidi, atapata zawadi nono."
Mke mmoja alienda sokoni akanunua nyama ya ng'ombe na viungo vingi.
Alirudi nyumbani na kupika kitoweo alichoamini kilikuwa kitamu.
Mke mwingine alienda soko iliyokuwa sehemu tofauti. Alinunua nyama ya pori pamoja na viungo tofauti.
Naye alirudi nyumbani kuitayarisha.
Mke wa mwisho aliamua kwenda kumuona mamake mfalme.
Aliambiwa apike chakula cha kienyeji na wala asiweke mafuta au viungo vyovyote vya kisasa.
Mke huyo wa tatu, alienda shambani kutafuta mboga tofauti za kutayarishia chakula cha kienyeji.
Mfalme na wenzake walifika kwa wake waliopika nyama ya ng'ombe na ya pori. Hata hivyo, mfalme hakukipenda chakula alichoandaliwa.
Walienda kwa mke aliyeandaa chakula cha kienyeji.
Mfalme alikifurahia sana kwani kilikuwa chakula alichokipenda. Alimteua mke huyo kuwa malkia katika ufalme wake.
Tangu siku hiyo, huyo mke aliheshimiwa sana. Yeye alijua namna ya kumfurahisha mmewe.

