Wimbo wa Sakima
Ursula Nafula
Peris Wachuka

Sakima aliishi na wazazi wake na dada yake mwenye umri wa miaka minne.

Waliishi katika shamba la mtu tajiri.

Nyumba yao ya nyasi ilikuwa mwisho wa safu ya miti iliyopendeza.

1

Sakima alipokuwa na umri wa miaka mitatu, aliugua na kupoteza uwezo wa kuona.

Hata hivyo, Sakima alikuwa na vipaji vya kipekee.

2

Sakima alitenda mambo mengi ambayo wavulana wengine wa umri wake hawakufanya.

Kwa mfano, angeketi na watu wazima na kujadiliana nao.

3

Wazazi wa Sakima walifanya kazi katika nyumba ya yule tajiri.

Waliondoka nyumbani asubuhi na mapema na kurudi jioni.

Sakima aliachwa na dadake.

4

Sakima alipenda kuimba nyimbo sana.

Siku moja mamake alimwuliza, "Sakima, unajifunza nyimbo hizi kutoka wapi?"

5

Sakima alimjibu, "Nazisikia akilini mwangu kisha naziimba."

Mama hakumwelewa mwanake.

6

Sakima alipenda kumwimbia dadake, hasa alipohisi njaa.

Dadake alimsikiliza na kucheza.

7

"Tafadhali Sakima, niimbie  tena," dada yake angemsihi.

Sakima angekubali na kumwiimbia mara nyingine.

8

Jioni moja, wazazi wake waliporudi nyumbani, walikuwa kimya sana.

Sakima alijua kwamba lazima kulikuwa na tukio baya.

9

"Kuna shida gani, mama, baba?" Sakima aliwauliza.

Sakima aligundua kwamba mwana wa tajiri wao alikuwa amepotea.

Tajiri alikuwa amehuzunika na kuhisi upweke mkubwa.

10

"Labda atafurahi tena nikimwimbia," Sakima aliwaambia wazazi wake.

Wazazi wake walidharau wazo lake. "Yeye ni tajiri. Wewe ni mvulana asiyeona. Wimbo wako utamsaidiaje?"

11

Hata hivyo, Sakima hakukata tamaa.

Dada yake vilevile alimpa moyo, "Nyimbo za Sakima hunituliza mimi nikiwa na njaa. Zitamtuliza tajiri pia."

12

Siku iliyofuata, Sakima alimwambia dadake amwongoze hadi kwenye nyumba ya yule tajiri.

13

Alisimama chini ya dirisha moja na kuanza kuimba wimbo wake alioupenda.

Polepole, kichwa cha yule tajiri kilianza kuonekana dirishani.

14

Wafanyakazi wote waliacha kazi zao wakamsikiliza Sakima.

Hata hivyo, mwanamme mmoja alisema, "Hakuna aliyefaulu kumtuliza bwana. Je, huyu mvulana asiyeona ataweza kumtuliza?"

15

Sakima alipomaliza kuimba wimbo wake alianza kuondoka.

Tajiri alitoka nje kwa haraka na kusema, "Tafadhali, imba wimbo wako tena."

16

Wakati huo huo, watu wawili walikuja wakiwa wamembeba mtu kwenye machela.

Walikuwa wamemkuta mwana wa tajiri akiwa amechapwa na kuachwa kando ya barabara.

17

Tajiri alifurahi sana kumwona mwanawe tena.   Alimzawadi Sakima kwa kumliwaza.

Aliwapeleka mwanawe na Sakima hosipitalini ili Sakima aweze kusaidiwa kuona tena.

18
You are free to download, copy, translate or adapt this story and use the illustrations as long as you attribute in the following way:
Wimbo wa Sakima
Author - Ursula Nafula
Illustration - Peris Wachuka
Language - Kiswahili
Level - First paragraphs