

Sikuwa nimewahi kuvaa viatu.
Nilipowaona watoto waliovaa viatu, niliwatazama kwa hamu.
Mamangu alinifariji akisema, "Utakuwa na jozi nyingi baadaye, subiri tu utaona!"
Wakati mwingine sikumwamini.
"Baadaye, itakuwa lini?" nilimwuliza siku moja.
Kisha ulikuwa msimu wa Krismasi. Kila mtu alijishughulisha kwenda sokoni na kurejea na vitu vipya.
"Mama, je, nasi tutaenda sokoni?" nilimwuliza.
Siku kabla ya Krismasi, mamangu aliniamsha mapema kuliko ilivyokuwa kawaida.
Alinieleza nilichukue lile kapu kubwa ambalo alilibeba kila alipokwenda sokoni.
Sokoni palikuwa na wazazi wengi walioandamana na watoto wao.
Walinunua nguo mpya na kiasi kikubwa cha vyakula.
Tulienda moja kwa moja hadi sehemu ya viatu aina tofauti.
Nilishangaa kwa kuona mstari baada ya mwingine wa viatu vilivyopangwa kwa unadhifu.
Baada ya kupima baadhi ya jozi nyingi, nilichukua jozi ya viatu vya michezo.
Sikuweza kulala usiku huo. Nilisisimkwa sana nilipowaza jinsi ningevivaa viatu vyangu vipya na kujivunia kila mtoto kijijini.
Muda mfupi baadaye, niliamka kitandani na kuvijaribu tena viatu vyangu.
Nilitembea polepole chumbani kisha nikavirejesha sandukuni.
Nilijaribu kulala lakini sikupata usingizi.
Niliamka na kuvijaribu tena kwa mara ya pili.
Nilitembea kwa maringo chumbani kisha nikavirejesha sandukuni.
Nilijaribu tena kulala nikinuia kupata usingizi. Lakini muda mfupi baadaye, niliamka kwa mara ya tatu.
Nilivivaa vyatu nikaruka ruka kidogo chumbani.
Nilihisi usingizi nikarudi kitandani.
Asubuhi yake, niliamshwa na mamangu.
"Hiki ni nini ninachoona?" aliniuliza.
Nilikuwa nimevaa viatu vyangu vipya kitandani!

